Omran Daqneesh ni mmoja wa watoto watano waliojeruhiwa vibaya katika mashambulio yaliyofanywa na ndege jana nchini Syria ambapo picha zinamwonyesha akiwa amejaa vumbi baada ya kutolewa katika kifusi kilichosababishwa na shambulio hilo.
Mtoto huyo ambaye anaonekana kutokuwa na fahamu na akiwa ametapakaa damu na akiwa amepakiwa katika gari la wagonjwa, ni kielelezo cha ukatili unaofanyika katika mji wa Aleppo nchini Syria katika vita vya ndani vinavyoendelea.
Picha za video zinamwonyesha akiwa amepata fahamu huku damu ikimtoka na akijaribu kupangusha vumbi usoni. Hata hivyo, anaendelea kusubiri ili kupata tiba kutoka kwa madaktari.
Taswira hizo za mtoto Omran zimeenea kwa haraka baada ya kuwekwa katika mitandao ya jamii jana, wakati ambapo juhudi za kidiplomasia zinafanywa ili kusimamisha mapigano hayo.
Mwanzoni mwa wiki hii, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, alionya kwamba mji wa Aleppo unakabiliwa na janga la kibinadamu hivi karibuni, na alizitaka Russia na Marekani kufikia makubaliano ya haraka ya kusimamisha mapigano katika mji huo na sehemu nyingine nchini humo.