The House of Favourite Newspapers

Mwalimu Mkuu Aanguka na Kufariki Akiwa Njiani Kuelekea Shuleni

0
Marehemu Lily Mbati

HALI ya huzuni ilitanda katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Shitoto iliyoko Mumias Mashariki, Kaunti ya Kakamega nchini Kenya baada ya mwalimu wao mkuu kuzirai na kufariki alipokuwa akielekea shuleni.

 

Akizungumza na moja ya vyombo vya habari, mtoto wake Edgar Akwabi alisema marehemu Lily Mbati ambaye alikuwa na ugonjwa wa kisukari alikuwa mzima usiku wa kuamkia jana.

 

“Nilizungumza na mama kwa simu na kumhimiza anywe dawa zake kama kawaida, na alinijibu kuwa atafanya hivo,” Akwabi alisema.

Baadaye alipigiwa simu asubuhi na majirani waliomjulisha kuwa mama yake alianguka akielekea kazini na kufariki.

 

Naibu wa Mbati, Ruth Musafu kwa upande wake alimkumbuka marehemu bosi wake kama kiongozi wa kutegemewa, aliyejitolea na aliyependa kazi ya ualimu.

 

“Sote tutamkumbuka sana. Tunaomba neema huku tukimuomboleza mkuu wetu mpendwa,” Musafu alisema.

 

Marehemu Mbati ndiye aliyekuwa mwalimu pekee wa somo la Sayansi ya Nyumbani katika shule hiyo.

Taasisi hiyo imeitaka Wizara ya Elimu kuliangalia suala hilo wanapojiandaa na mitihani ya kitaifa.

 

Mwili wa marehemu ulipelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali ya St Mary’s.

 

Haya yanajiri baada ya kifo cha Naibu wa mwalimu mkuu katika shule ya wasichana ya Migigo, ambapo mtoto wa marehemu mvulana alimuua mama yake katika hali isiyoeleweka. Hiki ni kisa cha pili mwezi huu kuhusu vifo vya walimu.

Leave A Reply