POLISI mkoani Mbeya imemrejesha mkoani humo mwanamama Atughanile Kalenga, ambaye alikamatwa jijini Dar es Salaam kwa amri ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila, akituhumiwa kutapeli viwanja vya watu na kuviuza kisha kwenda Ikulu na kumwambia Rais kuwa anatishiwa kuuawa.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Ulrich Matei, amemkabidhi mwanamke huyo kwa Chalamila wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika Mtaa wa Gombe ili ajibu tuhuma zinazomkabili.
Katika mkutano huo Chalamila amewaagiza polisi kuwatafuta watu wengine wanaodaiwa kushirikiana na mwanamke huyo kutapeli viwanja, akiwemo mumewe na aliyekuwa Ofisa Mtendaji wa Mtaa wa Gombe Kaskazini ambaye amehamia Kata ya Iganzo, Mbeya.
“Ikulu sio sehemu ya mzaha na kufanyia utapeli,” amesema Chalamila wakati akizungumza na wananchi hao.