NDITIYE AMFUKUZA MSIMAMIZI WA UJENZI WA BANDARI CHATO
NAIBU Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye, amemfukuza msimamizi wa ujenzi wa bandari ya Nyemirembe wilayani Chato mkoani Geita kwa kukosa sifa na utaalam wa kusimamia ujenzi wa bandari hiyo na miundombinu yake na kuagiza aondolewe mara moja kwenye eneo hilo
Hayo yamejitokeza wakati wa ziara yake ya kukagua hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa bandari hiyo na miundombinu yake ambapo mkandarasi wa kampuni ya V.J Mistry & Co. Ltd amepewa jukumu hilo na serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kujenga bandari hiyo kwa gharama ya shilingi bilioni 4.128.
Katika ziara hiyo, Nditiye amebaini kuwa msimamizi wa ujenzi wa bandari hiyo, Pravin Rabadhia wa wa kampuni ya V.J Mistry & Co. Ltd, hana utaalamu, sifa wala vigezo vyovyote vya kusimamia mradi huo unaogharimu matumizi ya fedha nyingi zinazotokana na fedha za makusanyo ya kodi ya wananchi.
Pia, alibaini uwepo wa Dipak Chaganlal, mfanyakazi wa kampuni hiyo aliyejitambulisha kwa Nditiye kuwa ana taaluma ya “storekeeper” akiwa msimamizi msaidizi wa mradi wa ujenzi wa bandari hiyo.
Nditiye alielekeza msimamizi huyo aondolewe eneo la mradi wa ujenzi wa bandari hiyo na mamlaka husika za vibali vya ajira, uhamiaji na mamlaka nyingine za manunuzi, bodi za makandarasi nchini zimchunguze taaluma yake, uraia wake, uhalali wake wa kufanya kazi ya kuwa msimamizi wa mradi huo kwa kuwa katika mahojiano naye akiwa kwenye eneo la mradi huo, wasimamizi hao wenye asilia ya Asia hawakuweza kutoa maelezo yoyote ya kitaalamu kuhusu maendeleo ya ujenzi wa bandari hiyo.
Nditiye ameelekeza kuwa kazi hiyo ya ujenzi wa bandari hiyo isimame kwa muda wa wiki moja na amemtaka mkandarasi wa kampuni hiyo kufika na kuripoti ofisini kwa Mkuu wa Mkoa wa Geita mara moja akiwa na wataalamu wanaohitajika kufanya kazi hiyo kuendana na matakwa ya mkataba husika na kuhakikisha kuwa wafanyakazi na vibarua wote wanalipwa fedha zao .
Comments are closed.