The House of Favourite Newspapers

Nkana Yawataka Yanga Wamsapoti Kessy

Hassan Kessy enzi akiwa Yanga.

NKANA FC inafahamu kwamba Yanga ina mashabiki wengi sana Bongo hivyo imeamua kuwatumia kwa kuwataka wajaze Uwanja wa Taifa kesho Jumapili ili wamsapoti beki wao wa zamani, Hassan Kessy katika mchezo dhidi ya Simba SC.

 

Simba kesho Jumapili watakuwa wenyeji wa Nkana katika mchezo wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa Afrika, katika mchezo wa kwanza uliopigwa wiki iliyopita kule Kitwe, Zambia, wenyeji Nkana walishinda mabao 2-1.

 

Kessy ambaye kwa sasa anachezea Nkana pia aliwahi kucheza Simba na baadaye Yanga kabla ya msimu huu kujiunga na Wazambia hao.

 

Kupitia ukarasa wa mtandao wa kijamii wa Facebook, uongozi wa Nkana FC umewaomba mashabiki wa Yanga kuisapoti timu hiyo katika kampeni yake ya kuiondoa Simba kwenye Ligi ya Mabingwa kutokana na uwepo wa Kessy aliyewahi kutumikia timu yao.

 

Taarifa hiyo ilisema kuwa: “Wapendwa mashabiki wa Yanga acha kwa sasa tuwe familia ya Nkana Yanga, Nkana pia ni timu yenu, jiungeni pamoja nasi wikiendi hii Dar es Saalam kwa kuipa sapoti Nkana ili iweze kuwaondoa Simba katika Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

“Lakini na mashabiki wa Yanga wakumbuke Kessy pia ni mtoto kutoka kwenye ardhi yao, wampe sapoti wikiendi hii,” ilisema taarifa hiyo.

Stori: Ibrahim Mussa, Championi Ijumaa

Comments are closed.