The House of Favourite Newspapers

Nkongo: Simba nendeni mkanishtaki Fifa

0

1

Mwamuzi, Israel Nkongo.

Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
BAADA ya kushushiwa shutuma nzito juu ya maamuzi yake katika mechi ya Simba dhidi ya Yanga, mwamuzi, Israel Nkongo ameibuka na kuwataka wanaoona hawakutendewa haki waweze kufika kwenye vyombo husika na kumshitaki ikiwemo kwenye Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).

Simba imekuwa ikilalama kuhusiana na kukandamizwa na Nkongo katika mechi hiyo iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar, wikiendi iliyopita na kufungwa mabao 2-0, huku Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara akithibitisha kuwa tayari jana wamewasilisha barua yao ya malalamiko kwenye Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF).

Katika mahojiano maalum aliyofanya na Championi Jumatano, Nkongo amefunguka kuwa kwa upande wake kanuni zinambana kuzungumzia mechi alizowahi kuwa mwamuzi, lakini kama timu yoyote itaona imeonewa na haikutendewa haki, basi inaweza kufuata ngazi muhimu na kumshitaki kwenye sehemu anazoweza kuchukuliwa hatua kubwa zaidi.

“Kanuni hazituruhusu kuzungumzia michezo niliyokwishaiamua huko nyuma, lakini nikwambie ule mchezo niliuchezesha kwa sheria, kanuni, taratibu na busara kama mwamuzi mwenye beji ya Fifa kwa kuwa ni mchezo mkubwa.

“Kama mtu ataona sikuwa sahihi au niliwakandamiza basi wanaweza kukusanya ushahidi na kufuata ngazi za kunishitaki kwenye vyombo husika vya juu hata Fifa,” alisema Nkongo.

Uongozi wa Simba pia umekuwa ukilalamika kuhusiana na kadi ya njano ya mapema ya beki wake, Juuko Murshid, kuhusiana na hilo bila kutaja jina, Nkongo anafafanua: “Mimi ni mwamuzi ‘senior’, mafunzo yangu yananiruhusu kuwasoma wachezaji ndani ya dakika 15 za mwanzo na kutambua nani anataka kuharibu mchezo, huyo nitakayembaini Fifa wanasema: ‘Destroy him, before he destroy your game’ na ndicho kilichotokea.”

Leave A Reply