The House of Favourite Newspapers

NMB yafuta tozo mbalimbali kwa wateja

Mkuu wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja, Abella Tarimo (kushoto) wa Benki ya NMB  akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Meneja Mwandamizi wa NMB, Bidhaa za Amana, Stephen Adili akizungumza. Katikati ni Mkuu wa Kitengo cha Akaunti na Malipo, Michael Mungure.

KATIKA kuharakisha kasi ya maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla, ikiwemo kuchagiza idadi ya Watanzania wanaotumia huduma za kibenki, Benki ya NMB imetangaza kufuta tozo mbalimbali kuanzia Februari mwaka huu.

Kufutwa kwa tozo hizo na kufungua milango ya huduma bure za kibenki ‘free banking,’ kumetangazwa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na Mkuu wa Kitengo cha Malipo na Akaunti wa NMB, Michael Mungure, alipoongea na wanahabari.

Mungure alibainisha kuwa, baada ya tafiti za kina, zilizojikita katika kujua kiini cha kutoongezeka kwa idadi ya Watanzania wanaotumia huduma za kibenki, hivyo kuachwa na kasi ya maendeleo kuelekea Uchumi wa Kati, wameamua kuja na ‘free banking.’

Alizitaja baadhi ya tozo zilizofutwa kuwa ni pamoja na ile ya kufungua akaunti kwa mteja mmoja mmoja (Individuals Account), ada ya kila mwezi (monthly maintenance fees), makato ya miamala (transactions fees) na kufufua akaunti ya zamani (dormant account).

“Hii tozo ya miamala tuliyofuta na ambayo itatumika kuanzia Februari mwaka huu ni ya kuhamisha fedha kutoka akaunti moja ya NMB kwenda akaunti nyingine ya NMB, lakini pia kutakuwa na huduma bure zilizotajwa hapo juu, pamoja kuuliza salio,” alisema Mungure.

Kwa upande wake, Meneja Mwandamizi wa Bidhaa za Amana wa NMB. Stephen Adili, aliwataka Watanzania kuchangamkia fursa ya kufutwa kwa tozo hizo kwa kufungua na kutumia huduma za NMB, ambazo zinapatikana kirahisi kidijitali pia.

“Kuanzia sasa tunataka wateja wetu na Watanzania kwa ujumla, waje wafungue akaunti kwa wingi na hakutakuwa na makato kama tulivyoainisha, fursa ambayo itaharakisha ustawi wa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla,” alisema Adili.

Comments are closed.