The House of Favourite Newspapers

Okwi Atangaza Hali ya Hatari Simba SC

Emmanuel Okwi

MSHAMBULIAJI wa Simba, Mganda, Emmanuel Okwi amesema kuwa hakuna atakayebaki salama mbele yao kwa kuhakikisha wanashinda mechi zao zote ili waweze kutetea ubingwa wa Ligi Kuu Bara.

 

Simba ina pointi 42, wakizidiwa pointi nane na Azam FC inayoshika nafasi ya pili ambapo timu hizo zinatarajiwa kukutana leo Ijumaa kwenye Uwanja wa Taifa, huku Yanga ikiwa kileleni kwa pointi 61.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Okwi alisema malengo yao ni kuhakikisha wanafanikiwa kutetea ubingwa wao kwa kushinda kila mchezo uliopo mbele yao ukiwemo wa leo.

 

“Sasa hivi tunaangalia mechi za mbele ikiwemo ya Azam, sisi hatuangalii zimebaki mechi ngapi, tunaangalia kushinda kila mechi baada ya nyingine kwa sababu tunachokitaka ni kupata pointi tatu.

 

“Kuifunga Yanga ni ushindi kama ulivyo ushindi wa kawaida, ndiyo ni derby lakini hilo lishapita na limebaki kwenye historia ila kwa kuwa tumemfunga, aliyekuwa juu yetu imeongeza kitu maana malengo ni kuchukua ubingwa,” alisema Okwi.

 

Upande wa afya yake Okwi amepona na yupo fiti baada ya kusumbuliwa na maumivu ya kifundo cha mguu wakati beki wa kati Juuko Murshid anasumbuliwa na maumivu ya ugoko. Meneja wa Simba, Patrick Rweyemamu amesema: “Okwi ana asilimia 100 ya kucheza dhidi ya Azam, Juuko bado hajawa fiti na uwezekano wa kuwepo kikosini ni mdogo.” Aidha, Rweyemamu alisema mshambuliaji Meddie Kagere anatarajiwa kuwepo kikosini baada ya kumaliza adhabu ya kadi tatu za njano.

Comments are closed.