The House of Favourite Newspapers

Orlando Pirates Yaifanyia Umafia Simba Bongo, Mashushushu Watumwa Kuwachunguza

0
Wachezaji wa Orlando Pirates.

IMEELEZWA kuwa mashushushu wa Orlando Pirates ya nchini Afrika Kusini, wapo nchini tangu wiki iliyopita wakiwafuatilia kwa ukaribu wapinzani wao, Simba.

 

Timu hizo zinatarajiwa kuvaana Jumapili hii katika mchezo wa kwanza wa Robo Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika utakaopigwa kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar.

 

Simba imevuka hatua hiyo ya robo baada ya kuwafunga US Gendarmerie ya nchini Niger mabao 4-0 ambao ulipigwa Uwanja wa Mkapa.

Kikosi cha timu ya Simba.

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatatu, Pirates wanatumia kila njia kuhakikisha wanapata ushindi wa ugenini kabla ya kwenda kurudiana nyumbani kwao Afrika Kusini.

 

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa mashushu hao walikuwepo kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga wakati timu hiyo ilipocheza mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Coastal Union ambao ulimalizika kwa Simba kushinda mabao 2-1.

 

Aliongeza kuwa mashushushu hao jana walitarajiwa kuwepo kwenye Uwanja wa Ushirika, Moshi wakati timu hiyo ikicheza dhidi ya Polisi Tanzania katika mchezo wa ligi kabla ya kukutana na Pirates.

 

“Uongozi wa Simba una taarifa za kuwepo nchini tangu wiki iliyopita viongozi wa Pirates waliofika kwa ajili ya kufuatilia michezo yetu miwili ya ligi dhidi ya Coastal na Polisi Tanzania.

 

“Hivyo tayari uongozi umechukua tahadhari za haraka zaidi ya mashushushu hao ili kuhakikisha tunatibua mipango yao ya ushindi hapa nyumbani,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, alisema: “Kama uongozi tunachukua tahadhari za haraka za kuharibu mipango ya mashushushu hao waliofika nchini kwa ajili ya kutufuatilia.

 

“Niwaondoe Wanasimba kuwa, licha ya kuwepo mashushushu hao lakini hawataweza kufanya chochote, kikubwa niwaombe mashabiki kujitokeza kwa wingi uwanjani kwa ajili ya kuishangilia timu itakapokuwa uwanjani.”

Stori Na Wilbert Molandi

Leave A Reply