The House of Favourite Newspapers

Rais Kenyatta Amuonya Mwanae kwa Kutoka Nje Usiku

0

 

RAIS wa Kenya Uhuru Kenyatta amefichua jinsi mtoto wake wa kiume alivyovunja marufuku ya kutotembea nje iliyowekwa nchini humo kuanzia saa moja jioni hadi saa kumi na moja alfajiri kuzuia kusambaa kwa virusi vya corona.

 

Alisema kuwa mmoja wa watoto wake wawili wa kiume, ambaye hakumtaja jina, hivi karibuni alikwenda katika sherehe usiku katika mji wa mwambao wa Kenya wa Mombasa-ambao ni kitovu cha maambukizi nchini Kenya. Mikusanyiko ya kijami hairuhusiwi katika taifa hilo lililoko Afrika Mashariki.

 

Serikali pia imezuia matembezi ya kuingia na kutoka katika mji mkuu , Nairobi, na katika kaunti nyingine tatu za eneo la mwambao, ikiwa ni pamoja na kaunti ya Mombasa, ambako familia yake rais pamoja na mama yake Mama Ngina Kenyatta wanaishi kwa sasa.

 

Katika mahojiano rais amesema kwamba hakuna aliye juu ya hatua za kudhibiti virusi vya corona, ingawa amekuwa akikosolewa kwa kutompeleka mototo wake katika kituo cha karantini sawa na Wakenya wengine wanaokiuka amri ya kutotoka nje wakati wa usiku.

 

Bwana Kenyatta alisema kuwa alimkanya kijana wake kwa kuhatarisha maisha ya bibi /nyanya yake Ngina Kenyatta:

‘Nikasema sawa umetoka nje na ukapata raha, lakini sasa umerudi kwa bibi yako mwenye miaka themanini na zaidi…kama chochote kitatokea kwa bibi yako kutokana na hilo ulilolifanya utaishi je …”, alinukuu mazungumzo aliyofanya na mtoto wake.

 

Mwenendo wa ugonjwa wa covid 19 nchini Kenya

Waziri wa Afya nchini Kenya Mutahi Kagwe siku ya Jumatano Mei 27 alitangaza watu 123 zaidi kuambukizwa virusi vya corona.

Hiyo ndiyo idadi kubwa zaidi ya maambukizi ya corona kuwahi kutangazwa kwa siku moja nchini humo tangu ugonjwa huo uingie Kenya mwezi Machi. Mpaka kufikia sasa Kenya imethibitisha watu 1,471 kuambukizwa virusi hivyo.

 

Wagonjwa hao wapya wanatokana na sampuli 3,077 ambazo zimepimwa hivi karibuni. Waziri Kagwe pia ametangaza watu watatu zaidi wamefariki kutokana na corona katika saa 24 zilizopita na kufanya watu waliopoteza Maisha kutokana na virusi hivyo nchini Kenya kufikia 55.

 

Bwana Kagwe ametangaza pia kuongezwa kwa muda wa udhibiti wa matembezi ya kuingia na kutoka katika maeneo ya Eastleigh jijini Nairobi na Makazi ya Old Town Mombasa. Kati ya wagonjwa hao wapya 123, jiji la Nairobi linaongoza kwa kuwa na wagonjwa 85 ikifuatiwa na 23 wa Mombasa.

 

Waziri Kagwe alieleza kuwa ongezeko hilo la wagonjwa linatokana na matumizi ya usafiri wa umma ambao ndio kimbilio la wengi nchini humo.

 

“Tumegundua kwamba watu wengi wamerejea katika namna ya usafiri wa awali, bila kujali kanuni za kujitenga na kanuni za uvaaji wa barakoa.”

 

Waziri Kagwe amewataka wananchi wa Kenya kuchukua hatua stahiki za kujilinda na kuwalinda watu wengine. “Haujui unakaa karibu na nani (kwenye gari). Na kulingana na takwimu tunazozipata, nafikiri.

 

itakuwa ni salama kudhani kuwa mtu uliyokaa ama kusimama karibu yake kuwa ana corona. Ukishaweka dhana hiyo, hautataka kuivua barakoa yako kwa kuwa utakuwa unajilinda.”

 

Kwa mujibu wa Kagwe, japo idadi ya maambukizi imepanda lakini kuna matumaini kwa Kenya. “…kwa ujumla wake, idadi hii ya maambukizi ni ndogo ukilinganisha na wengine na hususani idadi ya watu.

 

waliofariki kutokana na ugonjwa huu…Utaona ni idadi kubwa ya watu 123 lakini pia utaona idadi kubwa ya watu waliofanyiwa vipimo zaidi ya 3,000.”

Leave A Reply