Rais Samia Suluhu Hassan, leo Julai 22, 2021 amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza, Tony Blair ambaye pia ni Mwenyekiti Mtendaji wa Taasisi ya Tony Blair Institute of Global Change, ikulu jijini Dar es Salaam.
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Jaffar Haniu, inaeleza kuwa Blair amemhakikishia Rais Samia kuwa taasisi yake inaunga mkono jitihada mbalimbali anazochukua katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Tanzania.
Amesema katika kukabiliana na janga la Corona, taasisi yake ipo tayari kuisaidia Tanzania kwa kuwafikia wazalishaji wa chanjo hizo na kuongeza kuwa taasisi hiyo pia inawajengea uwezo nchi washirika kufuatilia miradi ya kilimo, nishati na matumizi ya teknolojia.
Kwa upande wake, Rais Samia amemshukuru Blair kwa kuitembelea Tanzania na kueleza kuwa serikali inaendelea na uboreshaji wa mazingira bora ya uwekezaji wa sekta binafsi ili kuwezesha utekelezaji wa mpango wa tatu wa maendeleo wa miaka mitano.