The House of Favourite Newspapers

Rais wa Zamani wa Sierra Leone ahojiwa kuhusiana madai ya jaribio la mapinduzi

0
Rais wa zamani wa Sierra Leone Ernest Bai Koroma

Rais wa zamani wa Sierra Leone Ernest Bai Koroma ameripoti katika kituo cha polisi katika mji mkuu wa nchi hiyo wa Freetown siku ya Ijumaa kuhojiwa kuhusiana na kile serikali ilichokiita jaribio la mapinduzi la mwishoni mwa mwezi Novemba, kwamujibu wa mwandishi wa shirika la habari la AFP.

Rais Koroma ambaye aliiongoza nchi hiyo ya Afrika Magharibi kwa miaka 11, mpaka mwaka 2018, aliwasili saa nne asubuhi kwa saa za huko katika idara upelelezi wa jinai akiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi na kusindikizwa na jeshi.

Wafuasi wake wachache walikuwa wakisubiri kuwasili kwake.

Muda wa mahojiano yake haukutajwa.

Rais Koroma siku ya Alhamis aliitwa kufika katika kituo cha polisi katika mji mkuu wa Freetown, ndani ya kipindi cha saa 24, ikiwa ni sehemu ya upelelezi unaoendelea kuhusiana na mapigano yaliyotokea mwishoni mwa mwezi uliopita.

Washambuliaji waliokuwa na silaha walivamia ghala ya silaha ya jeshi, kambi mbili, magereza mawili na vituo viwili vya polisi, walipambana na vikosi vya usalama nyakati za subuhi tarehe 26 mwezi Novemba.

Katika mapigano hayo watu 21 waliuwawa, kulingana na waziri wa habari Chernor Bah. Tangu wakati huo watu 71 wamekamatwa.

“Nitabaki kuwa muwazi na niko tayari kuusaidia upelelezi wa polisi kikamilifu” alisema Koroma katika taarifa siku ya Alhamisi .

“Acha sheria ifuate mkondo wake katika demokrasia yetu”

Ametoa wito wa utulivu na kuwataka wafuasi wake kuwasaidia polisi katika uchunguzi wao.

Afrika Magharibi imekumbwa na mfululizo wa mapinduzi tangu mwaka 2020 huku jeshi likichukua madaraka nchini Mali, Burkina Faso, Niger na Guinea.

Jumamosi, Rais wa Guinea-Bissau Umaro Sissoco Embalo alidai kunusurika na jaribio la mapinduzi baada ya mapambano kati ya jeshi na idara za usalama.

Leave A Reply