Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo imetimiza ahadi zake zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samiah Suluhu Hassan kwa kupeleka Vifaa Tiba Hospitali ya Wilaya ya Chalinze vyenye thamani ya Shilingi Milioni 480 ikiwemo mashine ya Kupiga picha za Mionzi yaani X-Ray, Jokofu la kuhifadhia maiti, mashine za kupimia damu na vifaa mbalimbali.
Mbunge wa Jimbo la Chalinze Mhe. Ridhiwan Kikwete ameishukuru serikali kwa kutekeleza ahadi hiyo ndani ya muda wa wiki tatu toka kutolewa kwa ahadi.
Kwa upande wao wananchi wa kata hiyo wakiongozwa na wakina mama ambao walikuwa wakivipokea wameshangilia huku wazee wakimuombea Mungu amlinde Rais wa Nchi yetu.
“Tunamshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu kwa kutusaidia vifaa tiba hivyo katika Hospitali yetu ya Wilaya, tulikuwa tukipoteza ndugu zetu kwa kukosa huduma mbalimbali zilizokuwa hazipatikani, aendelee kuwa na moyo huo, sisi wananchi wa chalinze tutaendelea kumuunga mkono ili aweze kutimiza malengo yake.
“Pia tunaendelea kujivunia kwa kuwa na mbunge makini ambaye amekuwa bega kwa bega nasi katika kutusemea changamoto zetu, tumekuwa mara kwa mara tukimuona akiwa Bungeni akiwasilisha kero zetu katika mhimili wa Bunge hivyo sisi wapiga kura wake wa Chalinze tunajivunia kwa kuwa na kiongozi makini, aendelee kupaza sauti zetu” walisema.