Sakata la Mume Aliyemuua Mke kwa Risasi Lawaibua Wanaharakati (Picha +Video)
MWANAHARAKATI Joyce Kiria ambaye kwa muda mrefu amekuwa akipambana kuhusu haki za wanawake na watoto ametembelea na kufanya mahojiano ndani ya Studio za Global Tv na +255 Global Radio katika Kipindi cha Mapito ambapo ameongelea mambo kadhaa kuhusu tukio lililotokea Mwanza la mwanamke Swalha kuuawa kikatili kwa kupigwa risasi saba na mumewe kutokana na kile kinachosemekana kuwa ni wivu wa mapenzi.
Kiria amesema umefika wakati sasa jamii itambue magumu wanayopitia wanawake na iachane na ile dhana ya kusema mwanamke avumilie mateso ya ndani ya ndoa, kwani imekuwa ni kasumba kwa wazazi na jamii kwa jumla kuwaambia wanawake wavumilie pale wanapokutana na matatizo ya ndani ya ndoa zao.
Mwanaharakati huyo pia amegusia juu ya tabia ya wanawake kuolewa kwa kufuata mali akibainisha kuwa jamii ya sasa mwanaume mwenye mali akioa anakuwa ameoa ukoo mzima na kutokana na jeuri ya kipato wanaume wengi wamekuwa wakiwanyanyasa wanawake.
Kiria amesema wanaume lazima wafundishwe kuwa kumuoa mwanamke siyo kummiliki kama gunia la mkaa kwani wanaume wengi wakitoa mahari wanachukulia kama wamenunua, amesisitiza lazima ifikie wakati itengenezwe jamii yenye usawa.
Mbali na hayo, Kiria ametoa rai kwa wanawake na jamii kwa jumla kupewa elimu kuhusu ukatili wa kijinsia na hasa mashuleni na nyumbani kuhakikisha kuwa wazazi wanawalea watoto katika malezi ya usawa kwani binadamu wote ni sawa na usawa wa kijinsia liwe suala mtambuka kwa kila mtu kwa kufanya hivyo matatizo haya ya ukatili wa kijinsia yatamalizika.
Kwa upande mwingine, msanii na mwanaharakati wa haki za wanawake ambaye ana Taasisi ya Voice of Women, Baby Madaha amesisitiza kuwa ifikie muda na wanaume nao wawe na taasisi zao za kuwasaidia kutatua changamoto za mahusiano yao kwani wanaume wengi wanabeba maumivu mengi yanayosababishwa na mahusiano na hawana kwa kuyapeleka tofauti na wanawake ambao wanazo sehemu nyingi za kusikilizwa matatizo yao.