SBL, Spika Ndugai waungana kupanda maelfu ya miti Kongwa
Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL), leo imeungana na viongozi pamoja na wananchi wa wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma katika zoezi la upandaji miti ikiwa ni sehemu ya mpango wa kampuni hiyo wa kutunza mazingira. Spika wa Bunge Job Ndugai na viongozi wa Halamashauri ya Wilaya ya Kongwa walikuwa ni badhi ya viongozi walioshiriki katika zoezi hilo la upandaji miti lililofadhiliwa na SBL.
Akiongea wakati wa zoezi hilo, mkurugenzi mtendaji wa SBL Mark Ocitti alisema upandaji miti katika wilaya ya Kongwa ni sehemu ya mkakati endelevu wa kampuni hiyo unaolenga kupanda maelfu ya miti sehemu mbali mbali hapa nchini.
Mkurugenzi huyo alisema mwaka 2019 kampuni ya SBL ilipanda miti katika wilaya za Same Pamoja na Moshi ili kuongeza uotokatika maeneo ya jirani na mlima Kilimanjaro.
“SBL inachukulia miti kama sehemu muhimu sana ya mazingira. Miti inasaidia kuhifadhi vyanzo vya maji, ni makazi kwa wanyama na wadudu mbali mbali, inavuta hewa chafu ya kaboni na kuzalisha hewa safi na pia miti ni chanzo cha dawa. Biashara yetu na jamii kwa ujumla ni sehemu ya mazingira na hii itunafanya kuwa jukumu letu sote kuyalinda na kuyatunza mazingira,” alisema Mark
Upandaji miti wa SBL unakuja katika kipndi ambacho dunia inahangaika kupunguza uzalishaji ya hewa ukaa ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabia ya nchi pamoja na kuyalinda mazingira kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo
Kwa upande wake Spika Ndugai aliishukuru kampuni ya SBL kwa kuunga mkono jitihada za upandaji miti na kuongeza kuwa miti ina nafasi ya kipikee kwa maisha ya watu na kusistiza kuwa bila miti hakuna maisha.
Ndugai alisema ukataji miti holela ni moja kati ya sababu za mabadiliko ya tabia ya nchi ambayo yamesababisha changamoto nyingi zinazomkabili binadamu ikiwa ni pamoja na athari kwenye uzalishaji wa chakula, upatikanaji wa maji, afya ya viumbe mbali mbali ikiwa ni pamoja na binadamu
Ni matumaini yangu kuwa zozei hili la upandaji miti litawavuta wakazi wengi wa Kongwa na maeneo mengine nchini kupanda miti kila wanapopata fursa. Pia napenda kuzikumbusha taasisi na makampuni mbali mbali kufikiria juu ya dunia yetu na kuchukua hatua za kuilinda na kuitunza,” alisema