The House of Favourite Newspapers

Serikali Ilivyojidhatiti Kupeleka Mawasiliano Vijijini

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako akifungua Mkutano wa Nne wa mwaka wa Mtandao Jamii mjini Dodoma jana (Jumatano, 30/10/2019). Mkutano huo wa siku sita ulioanza Jumatatu wiki hii (28/10/2019) umeandaliwa Jumuiya ya Mtandao wa Intaneti, the internet society (ISOC) kwa kushirikiana na Association for Progressive Communication (APC) na Chuo Kikuu cha Dodoma. 

SERIKALI ya Tanzania inatambua umuhimu wa kuwekeza katika mawasiliano kama mkakati mmoja wapo wa kuhakikisha azma ya kuwa nchi ya uchumi wa kati kupitia viwanda inafikiwa.

 

Hayo yameelezwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako alipomwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa katika ufunguzi wa Kongamano la Nne la Huduma ya Mtandao Jamii linalofanyika katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) ambapo amesema sekta ya mawasiliano ni moja ya sekta zinazochangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi nchini.

 

“Kwa kipindi cha Julai hadi Desemba 2017 sekta ya mawasiliano ilikua kwa asilimia 13.1 na ilikuwa sehemu ya pili katika kuchangia ukuaji wa uchumi nchini,” amesema Profesa Ndalichako.

Profesa Ndalichako amesema katika kuhakikisha huduma za mawasiliano zinafika mpaka vijijini, mwaka 2014 serikali iliingia mkataba na kampuni kutoka Vietnam wa kuhakikisha huduma hiyo inafika katika vijiji 4,000 ambapo kufikia Januari 2019, vijiji vyote vilikuwa vimefikiwa na huduma hiyo.

 

Waziri huyo ameendelea kuelezea kuwa serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) imefanya kazi kubwa katika kuhakikisha inafikisha mawasiliano vijijini ambapo mpaka sasa imeweza kupeleka huduma ya mawasiliano katika Kata 562 zenye vijiji 2,132.

Aidha, Profesa Ndalichako amesema kwa upande wa elimu, mfuko huo umewezesha kufika kwa huduma za mawasiliano katika baadhi ya shule na taasisi za kielimu pamoja na kutoa mafunzo ya huduma za mawasiliano kwa walimu wapato 1,229.

 

Akizungumza katika Kongamano hilo Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Profesa Faustine Bee amesema kongamano hilo linatoa nafasi kwa washiriki kujifunza namna ya kuendelea kuboresha huduma ya mawasiliano kwa jamii hasa jamii ambayo haijafikiwa na huduma hiyo.

“Lengo kubwa ni kuhakikisha ifikapo 2025 taasisi zote za serikali ziwe zimefikiwa na huduma ya mawasiliano ikiwemo vyuo vyote, shule zote za msi ngi na sekondari pamoja na ofisi zote za serikali,” amesema Profesa Bee.

 

Kongamano hilo la wiki moja linahusisha nchi za Afrika ambazo ni wanachama wa Internet Society Association for Progressive Community na ufanyika mara moja kwa mwaka, ambapo kwa mwaka huu limefanyika nchini Tanzania likiwa na washiriki kutoka Kenya, Uganda, Liberia, Cameroon, Ghana, Spain na mwenyeji Tanzania.

Comments are closed.