Serikali yadhamini vocha za pembejeo kwa wakulima
Kutoka kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi wa Pembejeo za Kilimo, Shenal S. Nyonni, Mkurugenzi wa Mazao, Twahir Nzalawahe na afisa habari wa wizara hiyo (anayezungumza kulia), Richard Kasuga.
Viongozi hao wakisikiliza maswali yaliyokuwa yakiulizwa na wanahabari (hawapo pichani).
Wanahabari wakifuatilia mkutano huo.
Waandishi wa habari wakichukua matukio.
SERIKALI kupitia Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika imetoa taarifa ya jinsi ilivyofanikiwa katika suala la kusambaza ruzuku ya pembejeo za kilimo kwa njia ya vocha katika msimu wa mwaka 2015/16.
Akizungumza na wanahabari katika Ukumbi wa Idara ya Habari (Maelezo) jijini Dar es Salaam, Afisa Habari wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Richard Kasuga amesema serikali imewawezesha wakulima wengi kupata pembejeo na kuwataka wote walionufaika na vocha hizo watambue kwamba serikali imewadhamini hivyo ni wajibu wao kuitumia vyema dhamana hiyo kwa maslahi yao na taifa.
Kasuga amesema wakulima wanatakiwa kuwa makini na ubora wa mbolea za mazao yao na kuhakikisha wanatumia ruzuku za pembejeo kwa kutumia vocha wanazopewa kwa lengo husika kuhakikisha wanazalisha mazao yenye ubora wa kimataifa.
Aliendelea kufafanua kuwa kutumia vocha hizo tofauti na madhumuni yaliyopangwa, kunapunguza uwezo wa taifa kujitosheleza kwa chakula hivyo ni lazima zitumike ipasavyo katika kuongeza uzalishaji wa mazao husika.
Kasuga ameeleza kuwa vocha 2,999,778 za pembejeo za kilimo zenye thamani ya shilingi bilioni 78.1 kuwa zimesambazwa katika mikoa 24 ya Tanzania isipokuwa Dar es Salaam pekee kwa ajili ya kufidia gharama za mbolea na mbegu bora katika msimu wa kilimo wa 2015-16 ambazo zitawanufaisha wakulima 999,926 wa mahindi na mpunga.
Vilevile amesema makampuni 23 ya mbolea na 27 ya mbegu bora za mahindi na mpunga yanaendelea kutoa huduma ya usambazaji wa pembejeo katika mikoa husika.
NA DENIS MTIMA/GPL
Mpango wa kutoa ruzuku kwa njia ya vocha utafanikiwa ikiwa mamlaka husika hususan Kamati za pembejeo zitafanyakazi kwa umakini katika ngazi zote kuanzia kijiji, kata, Wilaya, mkoa hadi Taifa.