The House of Favourite Newspapers

Sh Mil 150 Zampeleka Mkude Yanga

0

IMEFAHAMIKA kuwa mabosi wa Yanga wapo kwenye mazungumzo ya mwisho ya kuipata saini ya miaka miwili ya kiungo mkabaji wa Simba, Jonas Mkude kwa dau la Sh milioni 150 anazozitaka ili amwage wino Jangwani kwa siri.

 

Hiyo ikiwa ni siku chache tangu uongozi wa Simba umsimamishe kazi kiungo huyo kwa kile kilichotajwa utovu wa nidhamu ikiwa ni siku moja tangu timu hiyo itoke kucheza mchezo wake wa Azam Sports Federation Cup (maarufu kama Kombe la FA) dhidi ya Majimaji FC.

 

Kiungo huyo katika msimu wa 2018/2019 alikuwa anawaniwa vikali na Yanga kabla ya kuamua kubakia Simba kwa mkataba wa miaka miwili kwa dau la Sh milioni 100 alilowekewa mezani na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa klabu hiyo, Mohammed Dewji ‘Mo’.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatatu, kutoka ndani ya Kamati ya Usajili ya Yanga, kiungo huyo yeye mwenyewe amekubali kusaini mkataba wa kukipiga Jangwani baada ya kufi kia muafaka mzuri.

 

Mtoa taarifa huyo alisema mabosi wa Yanga na kiungo huyo wamekubaliana kuingia mkataba wa awali kwa dau hilo la Sh milioni 150 ambalo ametaka alipwe zote keshi huku akisisitiza kuwa amepanga kuondoka Simba mwishoni mwa msimu huu.

 

Aliongeza kuwa upo uwezekano mkubwa wa kiungo huyo kusaini mkataba wa miaka miwili ndani ya wiki mbili hizi mara baada ya kupatiwa fedha hizo ambazo anazitaka ili asaini.

 

“Mkude amebakisha miezi minne ili mkataba wake umalizike na kanuni za Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) zinaruhusu mchezaji kufanya mazungumzo na klabu nyingine itakayomhitaji kama akibakisha miezi sita.

 

“Hivyo mmoja wa mabosi wakubwa wa Kamati ya Usajili wa Yanga mwenye ushawishi ndiye anasimamia zoezi hilo zima la usajili na kama mambo yakienda vizuri, basi upo uwezekano wa kusaini mkataba wa awali ndani ya wiki mbili hizi.

 

“Hiyo ni baada ya kufi kia muafaka mzuri kati ya mabosi hao na mchezaji ambaye yeye tayari ametoa ofa yake ambayo ni shilingi milioni 150 ndiyo zitakazomfanya asaini mkataba huo wa miaka miwili ndani ya Yanga,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga ambaye ni Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM, Injinia Hersi Said hivi karibuni alitamba kwa kusema:

“Kama uongozi jukumu la usajili lote tumemuachia kocha wetu Kaze (Cedric) kwani ndiye anayependekeza usajili.

“Kama uongozi tukipokea mapendekezo ya usajili ya mchezaji yeyote atakayemhitaji kocha, sisi tupo tayari kutoa kiasi chochote, kikubwa kocha amhitaji tu.”

WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

 

Leave A Reply