MKURUGENZI Mtendaji wa Global Group, Eric James Shigongo, mapema leo alipata fursa ya kutoa somo la ujasiriamali katika semina iliyokuwa imeandaliwa na mmoja wa wakufunzi wa Chuo cha Tumaini kilichopo Mikocheni jijini Dar es Salaam, Dr. James Kazoka.
Akizungumza katika semina hiyo, Shigongo aliwaelimisha baadhi ya wanachuo waliokuwa wamehudhuria namna ya kutumia matatizo mbalimbali yaliyopo katika jamii kujipatia kipato kwani sehemu yoyote yenye matatizo mengi ndiyo mahali sahihi panapotoa fursa nyingi za kibiashara.
“Natambua watu wengi wangependa kuwa na mafanikio na hata kuwa matajiri, ila hawajui namna ya kutumia fursa katika baadhi ya jamii inayowazunguka kujipatia kipato kulingana na shida za mahali walipo.
“Kwa ujumla watu hufikiria kuwa tajiri lazima uanze na mtaji wa mamilioni ya fedha, jambo ambalo si kweli, lakini pia wengi wanaamini kuajiriwa pekee kunaweza kuwa njia sahihi ya kutengeneza fedha ya utajiri, jambo ambalo si kweli kwani siku zote aliyeleta mshahara alikadiria matumizi yako na kuufanya uishe kabla ya mwezi kufika.
“Napenda kutumia fursa hii kuwataka mtumie muda wenu wa ziada baada ya masomo au kazi kwani kwa kufanya hivyo mtaona mafanikio makubwa ambayo kwa namna moja mlikuwa mkiyapuuza,” alisema Shigongo.
NA MUSA MATEJA | GPL
Comments are closed.