The House of Favourite Newspapers

Haki za Binadamu Wataka Kifo cha Mwanamuziki Kuchunguzwa

0

SHIRIKA la kutetea Haki za Binadamu, Human Rights Watch linataka uchunguzi ufanywe kubaini chanzo cha kifo cha mwanamuziki maarufu wa nyimbo za injili nchini Rwanda, Kizito Mihigo. Mkurugenzi wa shirika hilo katika kanda ya Afrika ya kati, Lewis Mudge, ameiambia BBC kuwa shirika hilo linatilia shaka mazingira ya kifo chake na kwamba linataka uchunguzi huru ufanywe.

 

Mudge ameongeza kuwa Kizito alikuwa mwakilisha watu wanaojaribu kushinikiza mabadiliko nchi Rwanda miaka 26 baada ya mauaji ya kimbari.

”Hii sio mara ya kwanza watu kufariki wakiwa kizuizini au  kUuawa katika mazingira ya kutatanisha au kutoweka,” alisema Mudge akifafanua kauli yake.

 

Aliongezea kuwa mwaka 2018 mwanasiasa maarufu wa upinzani alitoweka akiwa jela na kwamba mamlaka ya jela wakati huo zilisema mwanasiasa huyo alikuwa akijaribu kutoroka lakini tangu wakati huo hajawahi kupatikana.

 

Mamlaka nchini Rwanda zinasema msani huyo alijiua alipokuwa anazuiliwa mahabusu katika kituo cha polisi. Kizito  alikuwa anazuiliwa kwa madai ya kujaribu kuvuka mpaka kiharamu kungia Burundi. Siku ya Jumatatu polisi ya Rwanda ilitangaza kwamba msanii huyo maarufu wa nyimbo za Injili, ”amejinyonga”.

 

Kwa mujibu wa tangazo hilo la polisi, maiti ya msanii huyo ilipatikana katika chumba alimokuwa anazuiliwa kwenye kituo cha polisi mtaa wa Remera, mjini Kigali.

 

Polisi imesema kwamba amejinyonga siku tatu baada ya kukamatwa karibu na mpaka baina ya Rwanda na Burundi katika kile ambacho polisi ilisema alikuwa na nia ya kutoroka nchi na kujiunga na makundi ya waasi dhidi ya Rwanda.

 

Wachunguzi nchini Rwanda wanasema kwamba uchunguzi kuhusu kifo chake umeanzishwa. Polisi wanasema kwamba Mihigo alijitoa uhai katika kisa kilichowashangaza mashabiki wake wengi na raia wa Rwanda.

 

”Uchunguzi umeanzishwa. mwili wake umepelekwa katika chumba cha karibu cha kuhifadhi maiti ambapo uchunguzi katika mwili wake utafanywa . Alikuwa akizuilia pekee katika kituo cha wachunguzi cha Rwanda katika eneo la Remera mji mkuu wa Kigali ambapo alipatikana amejinyonga ndani ya seli yake mapema alfajiri. Alitumia nguo aliokuwa anatumia kulalia kujinyonga”.

 

Hatahivyo wanaharakati wanaoishi ughaibuni wamepinga taarifa iliotolewa na polisi hao. Wamesema kwamba mwanamuziki huyo hakutaka kujiunga na kundi la waasi nchini Burundi na kwamba alitaka kwenda Ubelgiji ambapo alikuwa akiishi.

 

Pia wanaamini kwamba hakujiua katika kituo cha polisi alipokuwa anazuiliwa na kwamba huenda aliuawa. Muziki wa kizito ndio chanzo cha matatizo yaliomkumba . Katika wimbo mmoja alipendekeza kwamba kila mtu aliyeuawa katika mauaji ya kimbari ya 1994 anapaswa kukumbwa awe Mtutsi ama Muhutu.

 

Wanasema kwamba mamlaka imeliona hilo kama changamoto ya wazi dhidi yake na kwamba mauaji hayo yalitekelezwa na Watutsi. Wakosoaji wa serikali wanaamnini kwamba kutokana na hilo Kizito alilengwa.

 

Mwanamuziki huyo alikua ameanza kuchunguzwa kuhusiana na madai hayo pamoja na kutaka kuwahonga wananchi waliomkataa. Mwaka uliopita aliachiwa huru kwa msamaha wa rais baada ya kuhukumiwa kifungo cha miaka 10 jela kwa hatia ya kutaka kumuua rais na kuhamasisha raia kupinga serikali.

 

Kumekuwa na hisia mseto katika mitandao ya kijamii kuhusiana na kifo cha ghafla cha msanii huyo wa muziki wa injili huku baadhi ya watu wakitaka majibu kutoka kwa serikali. Kizito, aliyekuwa na miaka 38 alipata umaarufu kutokana na nyimbo zake kama vile ‘Inuma’ unaomaanisha njiwa na ‘Igisobanuri cy’urupfu’ ambao unaelezea kifo ni nini.

BBC Swahili

Leave A Reply