Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli amewaongoza waombolezaji na Watanzania wote kuaga mwili wa aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Eng. John William Herbert Kijazi katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es salaam.
Baada ya kuagwa kwa taratibu za kiserikali, mwili utasafirishwa hadi Korogwe mkoani Tanga ambapo atazikwa kesho Jumamosi.
Balozi Mhandisi Kijazi amekuwa mwakilishi wa Tanzania nchini India, Singapore, Sri Lanka, Bangladesh na Nepal mwenye makazi yake jijini New Delhi, India kuanzia mwaka 2007 – 2016 na hivyo kumfanya kuwa Mkuu wa Mabalozi wote wanaowakilisha Tanzania nje ya nchi.
“Kijazi ameondoka hapa Duniani kama shujaa, Maalim Seif ameondoka hapa duniani kama shujaa tuwaenzi na kuyaamini mambo yao waliyoyatekeleza hapa Duniani kwa mapenzi makubwa.
“Familia ya marehemu Kijazi, Mama Kijazi ninakuomba ukaendelee kulisimamia hili ninajua wewe nimuombaji mzuri endelea kumuombea mume wako, watoto mkaendelee kujenga umoja ulioachwa na Baba yenu, ndugu na jamaa akiwepo mdogo wake kasimamieni hilo.
“Nakushukuru Mzee Kikwete kwa kuja, nawashukuru viongozi wote mliohudhuria hapa nakushukuru sana Baba Poroko, Mungu ambariki sana marehemu Kijazi huko aendapko najua na sisi tuko njiani tunakuja, Mungu aibariki familia,” amesema Rais Magufuli.
Kabla ya kuwa balozi, Mhandisi Kijazi alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na baadaye Wizara ya Maendeleo ya Miundombinu kuanzia mwaka 2002 hadi 2006, baada ya kuteuliwa kuwa Balozi ndani ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano waKimataifa na hatimaye kupangiwa kituo cha New Delhi, India.