The House of Favourite Newspapers

Simba Yampa Dili nono Tshishimbi

MABOSI wa Yanga wameonekana kuvutiwa na kiwango kikubwa kinachoendelea kuonyeshwa na kiungo wao Papy Tshishimbi na kusababisha kuuweka mezani mkataba wake kwa ajili ya kuujadili.

 

Hiyo, ikiwa ni siku moja tangu kiungo huyo aonyeshe kiwango kikubwa katika michezo miwili ya Ligi Kuu Bara walipocheza na Simba kabla ya juzi kufanikisha ushindi wa mabao 2-1 walipovaana na Mbao FC kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza huku yeye akitoa pasi moja ya bao.

 

Kiungo huyo mwenye uwezo mkubwa wa kukaba na kuchezesha timu, amerejea uwanjani hivi karibuni akitokea kwenye majeraha ya goti aliyoyapata kwenye michezo iliyopita ya ligi.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo Championi Ijumaa, limezipata ni kuwa mabosi wanaohusika na usajili wa Yanga, tayari wameanza kufanya naye mazungumzo kwa ajili ya kumuongezea mkataba mwingine wa kuendelea kuichezea timu hiyo huku mchezo dhidi ya Simba ukitajwa mara kadhaa kuwa ndiyo ulikuwa chanzo.

Papy Tshishimbi.

Mtoa taarifa huyo alisema, viongozi wameanza mazungumzo na kiungo huyo baada ya kujadili mkataba wake na kugundua unamalizika, hivyo haraka wameanza mchakato huo wa kumbakisha kiungo huyo aliyerejea kwenye ubora.

 

“Tshishimbi alikuwa ameshasahaulika kwa viongozi na mashabiki wa Yanga, hiyo ni baada ya kutoonekana uwanjani kwenye baadhi ya mechi za ligi na Kombe la FA.

 

“Lakini katika michezo ya hivi karibuni aliyoicheza ya ligi ukiwemo na Simba na huu dhidi ya Mbao alionyesha kuwavutia viongozi na kuwashawishi kuanza naye mazungumzo kwa ajili ya kumuongezea mkataba mpya.

 

“Kila mtu alithibitisha ubora wa Tshishimbi baada ya mechi na Mbao, tofauti na kutengeneza bao alilolifunga Makambo (Heritier) alifanikisha kutawala safu ya kiungo kwa kupiga pasi nzuri na kukaba,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Alipoulizwa Zahera kuzungumzia hilo alisema: “Mara kadhaa nimekuwa nikimzungumzia Tshishimbi kutokana na aina yake ya uchezaji pale anapokosea na ninafanya hivyo ili abadilike kwa sababu nafahamu kiwango chake.

 

“Hivyo, bado ninaendelea kukifanyia tathimini kikosi changu katika michezo iliyobaki ya ligi na Kombe la FA kwa kuangalia mchezaji gani anayehitaji kubaki na kuondoka kwa wale ambao mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu, akiwemo Tshishimbi.”

Comments are closed.