Siri nzito kutumbuliwa kwa Mulongo
Rais John Maguful.
Na MWANDISHI WETU, RISASI MCHANGANYIKO
WAKATI pangua pangua ya nafasi za wakuu wa mikoa (RC) na wale wa wilaya (DC) ikiwa imekamilika juzi, siri nzito imegubika kufuatia kutenguliwa kwa uteuzi wa Mkuu wa Mkoa wa Mara, Magesa Mulongo kulikofanywa wiki iliyopita.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wananchi waliopiga simu chumba cha habari cha gazeti hili, walisema miongoni mwa viongozi ambao hawakuwa na shaka kuwa wangeendelea na nafasi zao ni Mulongo, hasa kwa kuwa alikuwa mchapakazi hodari.
Aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mara, Magesa Mulongo
“Sijui kwa kweli, huenda kwa vile Rais John Magufuli ndiye mwenye vigezo, lakini kama ni cha uchapa kazi na umri, nadhani huyu jamaa alikuwa anafiti kabisa, maana kila siku unasikia anavyowajibika hadi mtu unasema hapa tuna kiongozi, lakini kilichotokea kwa kweli siri nzito iko kwa mwenye nchi,” alisema Oscar Nelson, aliyepiga simu kutoka mkoani Mara.
Mwananchi mwingine aliyejitambulisha kwa jina moja la Mwajuma, akipiga simu kutoka Mwanza, alisema ameshtushwa sana na kuondolewa kazini kwa Mulongo, kwani alikuwa kiboko cha wabadhirifu na watumishi wavivu katika ofisi za umma.
“Ninamfahamu vizuri, alikuwa hapa Mwanza, kwa kweli kama ni kazi huyu ni mchapakazi, lakini mambo mengine nadhani rais ndiye anajua nini sababu ya kuondolewa kwake,” alisema mwanamama huyo.
Magesa Mulongo anakuwa mkuu wa mkoa wa pili kuondolewa kwenye nafasi yake tangu Rais John Magufuli awateue na kuwaapisha mapema mwaka huu. Wa kwanza alikuwa ni Anne Kilango Malecela, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, aliyefutwa uteuzi kwa kile kilichodaiwa kukubaliana na ripoti ya wasaidizi wake kuwa mkoa huo haukuwa na watumishi hewa.