The House of Favourite Newspapers

SKENDO YA KUMTAKA KIMAPENZI MCHUMBA’KE, HARMONIZE AMVAA BEN POL

DAR ES SALAAM: Kimewaka! Siku chache baada ya staa wa muziki wa Bongo Fleva, Benard Michael Paul Mnyang’anga ‘Ben Pol’ kuibuka na kudai kuwa kuna mastaa wanamtaka kimapenzi mchumba wake ambaye ni bilionea kutoka Kenya, Anerlisa Joseph Karanja Muigai, staa mwenzake, Rajab Abdul Kahali ‘Harmonize’ ameibuka na kumvaa, Gazeti la Ijumaa linakujuza.

 

Harmonize ni miongoni mwa mastaa waliotajwa na Ben Pol kuwa walikuwa wakimtokea mrembo huyo wakimtaka kimapenzi.

 

WALIPOANZIA

Hivi karibuni Ben Pol alifanyiwa mahojiano maalum na mtangazaji Zamaradi Mketema na kumtaja rapa Khaligraph Jones wa Kenya, Shetta na Harmonize wa Tanzania kuwa wamekuwa wakiwasiliana na mchumba wake kupitia ‘direct massage’ (DM) katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram.

“Kuna listi ya wasanii nimewaona meseji zao katika simu ya mchumba wangu, lakini wala hawanishangazi. Yupo Shetta, Harmonize na Khaligraph, sishangai kwa sababu (Anerlisa) ni msichana mrembo na ukipata nafasi ya kukaa naye kama hivi ndiyo unaona uzuri wake zaidi,” alisema Ben Pol.

 

HARMONIZE AMVAA

Wakati madai hayo yakiwa bado ya moto, Harmonize ameibuka na kusema ameumizwa na maneno aliyoyatoa Ben Pol kuwa anamtaka kimapenzi mchumba wake huyo. “Unajua mkiwa katika uhusiano, kila mtu anataka kumheshimu mwenzake kuwa usinichukulie poa, kuna mtu fulani alishawahi kunitongozaga. “Kuna vitu vingine vinaongelewa vinaweza kuwa vya ukweli au siyo kweli.

“Kwa hiyo ukiwa kama mwanaume rijali, ukisikia vitu kama hivyo si vizuri kuweka kwenye sehemu ya wazi. “Angeniambia tu, kaka shemela wenu kaniambia hivi na hivi na mimi ningemwambia hiyo si kweli,” Harmonize aliliambia Gazeti la Ijumaa na kuongeza;

 

“Lakini mimi namheshimu sana Ben Pol na sisi ni binadamu, wakati mwingine tunateleza. “Labda shemela wetu pia kaamua kusema hivyo kumwaminisha bro (Ben Pol) kuwa usinichukulie poa, kuna watu bado wananifuata kunitongoza. “Mimi nitakuwa mpumbavu kuona watu wako kwenye uhusiano siriazi halafu mimi namtumia meseji za kumtongoza DM.

 

“Ben Pol ni kaka yangu na ninampenda sana, nimeshiriki katika kazi yake ya Why (wimbo) na ninampenda kwa sababu ni mtu poa sana na ni mtu niliyekuwa nikipenda kuwa kama yeye, nimeanza kumsikia kipindi cha zamani nikiwa hata sijulikani,” alimaliza kusema Harmonize.

ANERLISA NI NANI?

Anerlisa ni binti wa miaka 31, anayetokea familia ya kitajiri akiwa ni mtoto wa kwanza ambapo mama yake, Tabitha Karanja anamiliki kiwanda kikubwa cha kutengeneza bia kiitwacho Keroche Breweries kinachosambaza vinywaji vyake sehemu kubwa ya nchini Kenya.

 

Baada ya kufanya kazi na mama yake kwenye kiwanda hicho cha bia, mwaka 2013, Anerlisa aliamua kufanya biashara ya kujitegemea kwa kuanzisha kampuni yake mwenyewe aliyoiita NERO inayojihusisha na kutengeneza maji ya kunywa yanayosambazwa sehemu kubwa ya nchini Kenya.

 

Kampuni hiyo ya NERO imempatia Anerlisa utajiri mkubwa alionao sasa. Kwa mujibu wa Jarida la Forbes lililotoka mwaka jana, Anerlisa ni miongoni mwa vijana 30 wanaokuja kwa kasi katika ujasiriamali Afrika na wanaotegemewa kuwa matajiri wakubwa.

 

Pia Jarida la Business Elites Africa linamtaja Anerlisa kuwa miongoni mwa matajiri Afrika wenye umri chini ya miaka 40 wanaokuja juu kwa kasi ya ajabu. Anerlisa anamiliki jumba la kifahari pande za Nairobi, magari kama yote yakiwemo Range Rover Evogue, Range Rover Velar na Jeep. Pia anamiliki vitu vya kifahari kama viatu aina ya Manolo Blahnik zaidi ya pea 100 vyenye thamani ya shilingi milioni mbili kwa pea moja.

WALIKUTANAJE?

Mwaka jana Anerlisa aliandaa shoo ya kuwapongeza watu wanaosapoti biashara yake ya maji ambapo mtumbuizaji alikuwa ni Ben Pol. Ilisemekana kuwa, baada ya shoo alimuomba Ben Pol wakatoe misaada kwenye kituo cha watoto yatima. Baada ya hapo ndipo mrembo huyo akatangaza kwa rafiki zake kuwa mchumba rasmi wa Ben Pol.

 

Katika Sherehe za Krismasi za mwaka uliopita, wawili hao walikwenda kujiachia kwenye mgahawa maarufu wa bei mbaya huko Dubai, Falme za Kiarabu. Mwezi Aprili, mwaka huu, Ben Pol alimvisha Anerlisa pete ya uchumba tayari kwa ndoa. Kwa sasa wameshafunga ndoa ya kimila ambapo sherehe zilifanyika hivi karibuni Runda Estate, Nairobi, Kenya.

Comments are closed.