The House of Favourite Newspapers

Straika Simba Aitwa Kenya

STRAIKA chipukizi wa Simba, Moses Kitandu, amepata dili la kujiunga na timu ya Nakumatt ya Kenya baada ya kuonyesha kiwango kizuri katika michuano ya SportPesa Super Cup, iliyoisha hivi karibuni nchini Kenya.

 

Kitandu ambaye ni miongoni mwa wachezaji vijana wa Simba ambao msimu wa 2017/18, walipandishwa kutoka timu ya vijana, alikuwa kwenye kikosi cha timu hiyo kilichomaliza nafasi ya pili kwenye michuano hiyo ambayo bingwa wake alikuwa Gor Mahia.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Kitandu alisema yupo tayari kujiunga na timu yoyote ikiwemo hiyo Nakumatt ambayo imeonyesha nia ya dhati ya kumhitaji.

 

“Ni kweli kuna timu kutoka Kenya ambayo ni Nakumatt imeonyesha nia ya kunihitaji nijiunge nayo, nitafanya hivyo endapo tu watafuata utaratibu kwa kuongea na viongozi wangu wa Simba kwani kwa sasa nipo kwenye mazungumzo na klabu yangu baada ya mkataba kumalizika.

 

“Mbali na hiyo, kuna timu nyingine zinazoshiriki ligi kuu ambazo ni Singida United, KMC na Coastal Union ambazo nazo pia zinanihitaji, kikubwa ninachoangalia ni maslahi yangu pamoja na ruhusa kutoka timu yangu ya Simba,” alisema Kitandu.

 

Championi Jumatano lilimtafuta Mjumbe wa Kamati ya Usajili ya Simba, Said Tully, kuzungumzia taratibu za kumruhusu mchezaji wao akitakiwa timu nyingine, ambapo alisema: “Tunajua kwamba katika wachezaji wetu wapo ambao hawapati nafasi kutokana na ushindani wa namba, hivyo basi kama kuna timu ina mahitaji na mchezaji yeyote kutoka kwetu kikubwa ni kufanya mazungumzo ili kuweza kumpa nafasi ya kuweza kuendeleza zaidi kipaji chake huko kwingine.”

STORI: LUNYAMADZO MLYUKA, Dar es Salaam

Comments are closed.