The House of Favourite Newspapers

Tanzania Yapokea Tuzo Ya Upatikanaji wa Umeme Vijijini

0
Meneja Miradi wa Kampuni ya Umeme ya Ensol, Prosper Magali (kushoto) akipokea tuzo ya kwa niamba ya serikali ya Tanzania kutoka Alliance for Rural Electrification yenye Makao Makuu yake nchini Ubelgiji .

Jitihada za Wizara ya Nishati na Madini za kuhakikisha umeme unafika na kusambaa maeneo ya vijijini zimetambuliwa kimataifa hali iliyopelekea Serikali kupokea Tuzo ya Uwezeshaji wa Mazingira Bora ya Upatikanaji wa Umeme Vijijini kwa Nchi zinazoendelea.

Serikali imetunukiwa Tuzo hiyo mwezi Machi, 22 na Taasisi ya Kimataifa ya Alliance for Rural Electrification yenye Makao Makuu yake nchini Ubelgiji ambayo ilipokelewa na Meneja Miradi wa Kampuni ya Umeme ya Ensol, Prosper Magali kwa niaba ya Serikali katika hafla ya utoaji tuzo iliyofanyika Lisbon, Ureno. Magali pia ni Makamu Mwenyekiti wa Taasisi ya Nishati Jadidifu (TAREA).

Wafanyakazi wa Kampuni ya Umeme ya Ensol wakikabidhi kwa pamoja tuzo hiyo kwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini anayeshughulikia Nishati, Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo (katikati).

Akikabidhi Tuzo hiyo Jijini Dar es Salaam, kwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini anayeshughulikia Nishati, Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo; Magali alisema Tuzo hiyo imetolewa kwa kutambua mchango wa Serikali ya Tanzania wa kufikisha huduma ya umeme maeneo ya vijijini pamoja na uwezeshaji wa mazingira bora na rafiki kwa wawekezaji wanaosambaza umeme katika maeneo ya vijijini.

“Kwa mwaka huu, Serikali yetu imetambuliwa kwa kufikisha umeme vijijini na juhudi zake za kuhakikisha kunakuwa na mzingira rafiki kwa watoaji na wasambazaji wa huduma ya umeme vijijini,” alisema Magali.


Kwa upande wake Dkt.Mhandisi Pallangyo aliipongeza kampuni ya Ensol kwa kupokea tuzo kwa niaba ya Serikali na kuahidi kuendeleza ushirikiano na kampuni zote zinazojihusisha na usambazaji wa umeme maeneo ya vijijini.
Alisema Serikali itaendelea kuandaa mazingira rafiki kwa wawekezaji ili kutimiza azma ya kuhakikisha vijiji vyote vinafikiwa na huduma ya Nishati ya Umeme.
Aidha, Dkt. Mhandisi Pallangyo alizitaka kampuni nyingine zinazoshughulika na uzalishaji na usambazaji wa umeme vijijini kujiunga na Taasisi za Kimataifa ikiwemo ya Alliance for Rural Electrification ili kunufaika na fursa zinazopatikana kwenye Taasisi hizo.
Makabidhiano hayo yalishuhudiwa na watendaji wa Wizara na Taasisi zake wakiongozwa na Kaimu Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli, Mhandisi Innocent Luoga na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Ensol, Hamis Mika

Leave A Reply