UN Yaipongeza Tanzania Kudhibiti Dawa Za Kulevya
SHIRIKA la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Dawa za Kulevya (CND) limeipongeza Tanzania kwa jitihada madhubuti katika kudhibiti na kupambana na tatizo la dawa za kulevya ambazo zimeleta matokeo chanya katika kipindi cha miaka mitatu mfululizo kuanzia mwaka 2018 hadi 2020.
Akizungumza na wanahabari leo makao makuu ya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Kivukoni jijini Dar leo, Kaimu Kamishna Jenerali wa mamlaka hiyo, James Wilbert Kaji, amesema pongezi hizo walizipata kwenye mkutano wa 63 wa Kamisheni ya Kimataifa ya Kudhibiti Dawa za Kulevya Duniani (CND) uliofanyika Vienna – Austria.
Amesema Mkuu wa CND Bi. Ghada Fathi Wally ameitaja Tanzania kuwa ni kati ya nchi chache barani Afrika zilizofanikiwa kupunguza madhara yanayosababishwa na matumizi ya dawa hizo.
Pamoja na jitihada zote mpaka kuifikia hatua ya kupongezwa na Umoja wa Mataifa, Kaji ameelezea masikitiko yake kwa vyombo vya habari vinavyoandika habari za uzushi kuhusu mapambano ya dawa hizo na kusema eti, Tanzania ndiyo kitovu cha dawa za kulevya Afrika Mashariki.
Akikanusha habari hizo amesema kimataifa nchi yetu imekuwa mfano wa kuigwa kwani hata nchi za Uganda, Msumbiji, Ghana, Nigeria na Norway zimeomba kujifunza kutoka hapa Tanzania na kutaka kujua mbinu za utendaji kazi na jinsi sheria yetu inavyofanya kazi.
HABARI:NEEMA ADRIAN
PICHA: RICHARD BUKOS/GPL