The House of Favourite Newspapers

Tshabalala Aanza Jeuri Simba

NAHODHA Msaidizi wa Simba, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ amesema ushindi wa mabao 3-1 walioupata dhidi ya JKT Tanzania, wiki iliyopita umerudisha morali kwa wachezaji hadi kwa mashabiki wa timu hiyo.

 

Simba ilifanikiwa kupata ushindi huo ukiwa mchezo wao wa kwanza wa Ligi Kuu Bara msimu huu uliopigwa kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Tshabalala alisema kitendo cha wao kuondolewa kwenye Raundi ya Awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika walipocheza dhidi ya UD Songo ya Msumbiji kilisababisha wachezaji wajione wana deni kubwa kwa mashabiki.

 

Tshabalala aliongeza kuwa, ushindi huo walioupata na JKT utawarejesha wachezaji katika hali ya kawaida na kuendelea kufanya vizuri katika michezo ijayo ya ligi.

 

“Tunafahamu kitendo cha kuondolewa kwenye michuano ya kimataifa kimewakera mashabiki wetu, kiukweli ni matokeo ambayo hatukuyatarajia, kwani sisi tumeumia.

“Hivyo, tumehamisha nguvu zetu kwenye ligi na tunashukuru tumepata ushindi wa muhimu katika mchezo wetu wa kwanza kwa kuwafunga JKT mabao 3-1.

 

“Ninaamini kuwa morali itakuwa imerejea kwa wachezaji na mashabiki ambao waliumia baada ya kuondolewa Caf, niwatake mashabiki kuendelea kutusapoti katika michezo ijayo ya ligi ili tufanikishe malengo yetu,” alisema Tshabalala.

Comments are closed.