The House of Favourite Newspapers

Usipige Bwana…Tuma Meseji!-3

1

ILIPOISHIA GAZETI LA IJUMAA:
“Utaishi tu. Si ndiyo maana amekuacha kwangu shem, alijua unaweza kukosa hata pesa ya kula, mimi nipo, utakula. Unaweza kukosa pesa ya kuweka mafuta kwenye gari, mimi nipo…”
“Shemeji ninachosemea mimi nitaishije ni tofauti na vyote hivyo ulivyovisema wewe,” alifunguka Aisha…TAMBAA NAYO…

Bony alimtumbulia macho ya mshangao Aisha kisha akasema…
“Una maana gani shemeji yangu?”
“Mh! Shemeji bwana… haiwezekani ukawa haujanielewa… sasa yeye yuko mbali na mimi na mimi ni mwanamke mwenye afya njema, hisia nzuri, unadhani nitaishije bila yeye?”
“Ahaa! Sasa wewe shemeji ulitakaje, jamaa arudi Bongo?”

“Wala! Si amekwenda kikazi bwana,” alisema Aisha, mara simu yake ikaita…
“Neema huyo anapiga,” alisema Aisha.
Kwa vile alikuwa anakula, aliiweka sauti ya nje ‘loud speaker’ ili azungumze…
“Ee, Neema vipi?”
“Poa, umeshaamka?”

“Ndiyo kwanza nakunywa chai na mume wangu hapa…”
“Afadhali unisaidie, maana kwenye kunywa chai huyo ni msumbufu sana.”
“Hata mimi namuona, hivi nimemwambia hapa hawezi kusimama mpaka amalize chai yote na mikate na mayai yake,” alisema Aisha, Neema akacheka sana kisha akaagana na Aisha na kukata simu…

“Kwa hiyo mnapeana kazi ya kunilazimisha kunywa chai na mke mwenzako siyo?”
“Ndiyo maana yake,” alikubali Aisha huku akimwangalia Bony kwa jicho la kuibia kwa mbali…
“Da! Mwaka huu nisiponenepa basi tena! Yaani jinsi wake zangu mnavyonipenda…Teh! Teh! Teh!” alisema Bony huku akichekacheka…

“Eee! Tena inabidi tuweke zamuzamu, mimi zamu yangu hata ikiwa mara mbili tu kwa wiki moja inatosha sana,” alisema Aisha kwa sauti iliyoashiria kuelemewa na jambo moyoni badala ya kuashiria utani…

“We ulie tu…na si ajabu jamaa kule Ulaya akaamua kuoa tena. We kwako itafuatia talaka tu urudi kwenu.”
Bony hakujua kama maneno hayo yalikuwa yakimzunguka kichwani Aisha, palepale kwenye kunywa chai akaanza kumwaga chozi na kuachana na chai…
“He! Shemeji, imekuaje tena?” aliuliza Bony naye akiacha chai na kusimama, akamfuata Aisha kwenye kiti…

“Shemeji vipi tena?”
“Hakuna kitu shemeji,” alisema Aisha, akasimama lakini hakutembea…
“Shemeji, au unaumwa?”
“Hapana…”

“Nimwite Neema basi kama umejisikia vibaya ghafla?”
“Hapana shemeji, mwache aendelee na kazi tu.”
“Sasa nini kinakuliza shemeji yangu wakati tulikuwa tunaongea vizuri?”
“Maneno yako yamenichoma sana… unajua shem hata mimi nimekuwa nikiwaza kwamba, huenda Mudy akaoa mwanamke mwingine kule wa Kizungu…sasa wewe uliposema vile ndiyo nikashtuka kwa nini uzungumze jambo ambalo na mimi linanitesa?”

“Ooo! Shem, amini…Mudy ni rafiki yangu tangu utotoni. Hana ujinga huo! Hilo haliwezekani hata siku moja shemeji. Kuwa na amani ya moyo, mimi nipo nitakupigania mpaka mwisho,” alisema Bony kwa utulivu.

Aisha aliinua uso na kumwangalia Bony, akaachia tabasamu la mbali kisha akainua mikono na kumkumbatia Bony…

“Niliogopa sana shem kama Mudy anaweza kuoa. Afadhali umenipa neno lenye kunipa matumaini sasa,” alisema Aisha akiwa ameacha kumkumbatia shemejiye huyo…
“Kuwa mpole Aisha. Mimi ni mimi, sitakuja kukaa hata siku moja nione Mudy amekuacha na haitatokea Mudy akakuacha. Niamini mimi.”

Maneno hayo yalizidi kumpa nguvu Aisha na kuanza kumwona Bony kwamba kumbe ndiye aliyeshikilia ndoa yake. Alizidi kumuweka moyoni mwake…

“Nimefurahi sana shemeji… nakutegemea wewe,” alisema Aisha akamsogelea Bony na kumbusu.
Bony akaweka uswahili pembeni, akaingiza uzungu ndani, naye akambusu…akambusu…akambusu tena. Lilikuwa busu la pande tatu shavu la kulia, kushoto na kwenye paji la uso!
Mabusu hayo yalimsisimua Aisha, akajikuta amemkodolea macho Bony huku akimwambia…
“Shemeji sitaki huko.”

“Hutaki nini..?”
“Kunipa mabusu.”
“Aaah! Sasa wewe mke gani hujui kupigwa mabusu…hebu pokea na hilo,” alisema Bony na kumpiga busu jingine la nguvu zaidi.

Je, nini kiliendelea hapo? Usikose kusoma chombezo hili jipya kwenye Gazeti la Ijumaa, Ijumaa ijayo.

1 Comment
  1. alex rodrick says

    tayali embe imeshaiva

Leave A Reply