The House of Favourite Newspapers

Uwanja tu, Simba SC Inamwaga 500,000 Kila Siku

OFISA Mtendaji Mkuu wa Simba, Senzo Mazingisa, raia wa Afrika Kusini, amefunguka kuwa wanapambana kuhakikisha wanakamilisha ujenzi wao wa Bunju Complex kwa lengo la kupunguza matumizi makubwa ya fedha yanayofikia hadi Sh milioni 15 kwa mwezi.

 

Bosi huyo amesema wamekuwa wakitoa Sh 500,000 kila siku kwa ajili ya kulipia uwanja wa mazoezi ambayo ikuupiga kwa mwezi ni karibu milioni 15.

 

Simba inapambana kukamilisha ujenzi wa uwanja huo uliopo Bunju B nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam, kwa ajili ya kuanza kutumika katika mazoezi ya timu hiyo inayoshiriki Ligi Kuu Bara na Kombe la FA.

 

Mazingisa kwa sasa anapambana kupunguza gharama za matumizi kwa timu hiyo ili kuweza kwenda katika mfumo wa kisasa akiwa na rekodi ya kufanya kazi na klabu kubwa za Afrika Kusini ikiwemo Platnumz Stars na Orlando Pirates ‘Buccaneers’ zinayoshiriki ligi kuu ya nchi hiyo, maarufu kama PSL.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu katika mahojiano maalum, Mazingisa alisema kuwa wanapambana kukamilisha ujenzi wa viwanja vyao ifikapo Desemba, mwaka huu kwa lengo la kupunguza gharama za matumizi.

 

Bosi huyo ambaye yupo makini na majukumu yake, amesema: “Tungekuwa tumeshakamilisha, lakini kila mara tunapofanya kitu, mvua inanyesha. Mvua imetukwamisha sana, imeharibu kazi tuliyofanya na ikinyesha inakurudisha nyuma, huwezi kufanya chochote. Ukiangalia kama ule uwanja wa nyasi bandia umevurugika kiasi.

 

“Umekosa usawa katika eneo la kutandika kapeti ya nyasi kwa sababu ya hizi mvua, yaani umekuwa na mabonde mabonde, unahitajika kuwekwa sawa upya kabla ya kutandika nyasi na tumeona tusubirie kidogo hali ya mvua ziishe kabla ya kuendelea.

“Unajua tunatumia gharama kubwa kiasi gani kulipia uwanja wa mazoezi?

 

Kwa siku ni shilingi laki tano, ndani ya wiki si chini ya milioni 2.5, piga kwa mwezi ni Sh ngapi na kwa mwaka. Ni pesa nyingi ambayo tunatumia, japokuwa ule uwanja wetu wa nyasi umebaki sehemu ndogo kule Bunju kukamilika,” alisema Mazingisa.

 

Ikumbukwe Simba inajenga viwanja viwili vya mazoezi ambapo kutakuwa na uwanja wenye nyasi za asili ambao umebaki sehemu ndogo kukamilika na wa nyasi bandia ambao bado haujakamilika huku ukijumuisha hosteli zitakazokuwa kwenye eneo hilo.

 

Kwa sasa Simba inalazimika kutumia viwanja vya kukodi huku wakilipia shilingi laki tano kwa siku ambapo wamekuwa wakitumia Uwanja wa Gymkhana na Uhuru kwa nyakati tofauti.

 

IBRAHIM MUSSA NA MARTHA MBOMA

Comments are closed.