Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan amejumuika na viongozi, wasanii na mamia ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam kuuaga mwili wa aliyekuwa mke wa Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo Dk Harrison Mwakyembe, Linah Mwakyembe.
Mke wa Waziri Mwakyembe alifariki dunia juzi kwa maradhi ya saratani ya titi.
Akitoa salamu kwa niaba ya serikali leo Jumanne Julai 18, Mama Samia amemtaka Dk Mwakyembe kuwa mvumilivu katika kipindi hiki kigumu.
Amesema: “Tunafahamu kama umempoteza mtu muhimu sana kwako lakini unatakiwa kuwa mvumilivu na kuendelea kumshukuru Mungu kwa hilo, kwa upande wa Serikali tunatoa pole nyingi.”
Pamoja na Makamu wa Rais walikuwepo pia viongozi wastaafu wa Serikali, marais Benjamin Mkapa na Mzee Ali Hassan Mwinyi.
Pia walikuwapo viongozi waandamizi wa Serikali, mawaziri, wabunge, wanasiasa, viongozi wa michezo, wasanii na wanahabari.
Marehemu Linah Mwakyembe Alivyoagwa Dar
Kwa upande wake Waziri wa Sheria na Katiba, Profesa Palamagamba Kabudi amempongeza, Dk Mwakyembe kwa kutimiza majukumu yake ya kazi ilhali alikuwa akiuguliwa.
“Licha ya kuuguliwa na mkeo mpenzi, uliendelea na majukumu yako kwa jitihada na uaminifu mkubwa, unastahili pongezi,”amesema.
Akiendesha ibada ya mazishi iliyofanyika katika Kanisa la KKKT Usharika wa Kunduchi, Msaidizi wa Askofu Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Chediel Lwiza amesisitiza Watanzania kuishi kwa kumtumikia Mungu.
“Mama Mwakyembe alitoa maisha yake kwa ajili ya kanisa, alishiriki shughuli mbalimbali, alijitoa kwa moyo wake wote, tunapaswa kufuata mfano huo, yeye amemaliza kazi tubaki na ujumbe huo,” amesema.
PICHA ZOTE NA ISSA MNALLY | GPL