The House of Favourite Newspapers

Virusi vya Corona Vyamuua Daktari Aliyevibaini

0

 

DAKTARI mmoja nchini China aliyejaribu kutoa taarifa ya kwanza ya kuwapo mlipuko wa virusi vya Corona amekufa kutokana na maambukizo ya virusi hivyo.

Vyombo vya habari vya China vimenukuliwa na BBC vikisema Li Wenliang alikuwa daktari wa macho katika Hospitali ya Wuhan Central, alipobaini na kutuma taarifa ya mlipuko huo kwa madaktari wenzake Desemba 30, mwaka jana.

Baada ya taarifa hiyo, polisi walimwita na kumuonya aache, wakati mamlaka za serikali zilikuwa zikitaka kuzuia taarifa hizo.

Virusi hivyo hadi sasa vimeua watu 560 na kuambukiza wengine 28,000 nchini China. Daktari huyo alichapisha taarifa yake kwenye mtandao wa Weibo akiwa kitandani, mwezi mmoja baada ya kutoa taarifa za awali za kuwapo kwa virusi hivyo.

Dk. Li (34) alikuwa ameona wagonjwa saba wenye maambukizi ya virusi alivyofananisha na ugonjwa wa sars, virusi ambavyo vilitangazwa janga la dharura kwa dunia mwaka 2003. Desemba 30 alituma ujumbe kwenye kundi la madaktari wenzake, akiwatahadharisha wavae mavazi ya kujikinga na maambukizi.

Siku nne baadaye aliitwa na idara ya usalama ya China na kutakiwa kusaini barua iliyomtuhumu “Kuchapisha taarifa za uongo ambazo zilisababisha usumbufu kwa jamii”.

Dk Li alikuwa miongoni mwa watu wanane ambao polisi walisema wanachunguzwa kwa kusambaza uvumi. Mamlaka za eneo hilo baadaye zilimwomba radhi Dk Li.

Katika taarifa yake kwenye Weibo, anasema jinsi alivyoanza kukohoa Januari 10, siku iliyofuata akapata homa na siku mbili baadaye akalazwa hospitalini.

 

Alipopimwa Januari 30 ikabainika anasumbuliwa na virusi vya Corona. Taarifa mbalimbali kwenye mitandao ya kijamii ya China zimeeleza masikitiko kutokana na kifo chake.

Leave A Reply