The House of Favourite Newspapers

Wafanyakazi SBL Wapanda Mlima Kilimanjaro Kuhamasisha Utalii wa Ndani

0
Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Mark Ocitti (wa kwanza kushoto), akizungumza na wafanyakazi 28 wa kampuni hiyo wakati wa uzinduzi wa kampeni yao ya kutangaza utalii wa ndani kwa kupanda Mlima Kilimanjaro iliyoanzishwa na SBL Agosti 14. Kampeni hiyo pia ni sehemu ya mpango ya kampuni ya kujenga afya ya kimwili na ustawi kwa wafanyakazi wake wakiwa kazini.

 

 

Machame Kilimanjaro, Agosti 14. Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) chini ya chapa yake mama ya ‘Serengeti’ imeunga mkono juhudi za Rais wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kupitia kampeni ya Royal Tour kwa wafanyakazi wake kupanda Mlima Kilimanjaro, mlima mrefu zaidi barani Afrika.

 

Pamoja na kuhamasisha utalii wa ndani, zoezi hilo la kupanda mlima Kilimanjaro pia ni sehemu ya programu za kampuni hiyo kujenga afya ya mwili kwa wafanyakazi wake kupitia kufanya mazoezi.

Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Mark Ocitti (wa kwanza kulia) akitoa ishara ya kuzindua kampeni ya kuhamasisha utalii wa ndani kwa kupanda mlima Kilimanjaro kwa wafanyakazi 28 wa kampuni hio tarehe 14 Agosti mkoani Kilimanjaro. Zoezi hilo la kupanda mlima pia ni sehemu ya programu za kampuni hiyo kujenga afya ya mwili kwa wafanyakazi wake kupitia kufanya mazoezi wakitarajiwa kushuka tarehe 20 Agosti.

 

 

Safari ya kupanda mita 5,895 za mlima Kilimanjaro ilianza Agosti 14 katika lango la Machame na jumla ya wafanyakazi 28 wa SBL kutoka viwanda vyao vilivyopo Mwanza, Moshi, na Dar es Salaam wameshiriki, huku wakitarajiwa kushuka Agosti 20.

 

Kabla ya kuanza kwa zoezi hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Mark Ocitti alisema, “Tanzania imejaliwa kuwa na maliasili nyingi zenye mvuto wa pekee kwa ajili ya utalii.” Hivyo basi, inatupa hamasa ya kuunga mkono kampeni ya Royal Tour ya Mheshimiwa Rais. Aidha, zoezi hili ni la makusudi la kuiweka chapa yetu ya Serengeti Trademark katika kilele cha Mlima Kilimanjaro.’’

 

Ocitti aliendelea, “Hii itakuwa ni kampeni endelevu ambapo tutakuwa tunatembelea vivutio mbalimbali nchini Tanzania ili kuchochea jitihada za kimakusudi za kukuza uchumi wetu kupitia utalii wa ndani. Tutakuwa tukifanya utaratibu huu pia kama njia mojawapo za kulinda afya za wafanyakazi wetu na kuwafanya wafurahie maisha wakati wowote na popote watakapokuwa’’.

 

Baadhi ya wafanyakazi wa Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya kupanda Mlima Kilimanjaro katika kampeni yao ya kuhamasisha utalii wa ndani na afya ya mwili na akili sehemu za kazi. Safari yao ilianza Agosti 14 katika lango la Machame ikiwa na wafanyakazi 28 wa SBL kutoka viwanda vya kutengeneza bia vya Mwanza, Moshi, na Dar es Salaam, huku wakitarajiwa kushuka Agosti 20.

 

 

Mmoja wa wafanyakazi, Rispa Hatibu, alinukuliwa akisema, “tuna shauku kubwa kuupanda mlima huu mrefu barani Afrika. Tunafahamu safari haitokuwa rahisi, itakuwa na uchovu mwingi ila kila mmoja wetu tumedhamiria kufika kilele cha Afrika.’’

 

Zoezi la wafanyakazi wa SBL ya kupanda Mlima Kilimnjaro inakuja kwa wakati Serikali imeweka mkakati wa  kukusanya mapato ya dola bilioni 6 kutoka kwa utalii ifikapo 2025 kwa kufikia watalii milioni tano kwa mwaka. Halikadhalika, ripoti zinaonyesha kuwa idadi ya watalii itavuka idadi ya watu milioni moja ifikapo mwisho wa mwaka huu baada ya kushuka hadi 600,000 mnamo 2020 kutoka milioni 1.5 mnamo 2019.

Leave A Reply