The House of Favourite Newspapers

Wanaoficha fedha ni wahujumu uchumi – Wasomi

0

ProfesaBanaMhadhiri Mwandamizi wa Masuala ya Uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana.

KUTOKANA na kauli ya Rais John Magufuli aliyoitoa juzi jijini Dar es Salaam kuwa anafahamu wapo wananchi wameficha fedha nyumbani, wachumi wametoa maoni yao na kusema hao ni wahujumu uchumi na wanapaswa kutafutwa na vyombo vya dola na washtakiwe.

Akitoa maoni yake jana jijini Dar Salaam, Mhadhiri Mwandamizi wa Masuala ya Uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana alisema uhai wa uchumi ni uwepo wa mzunguko wa fedha za kutosha.

Dk Bana alisema uchumi wa taifa lolote ni lazima katika kazi na shughuli za kimaendeleo na kijamii fedha ziwepo ili kufanya mzunguko uongezeke na kukuza uchumi, lakini uchumi huathirika iwapo kutatokea watu wanauhujumu kwa njia mbalimbali.

“Baadhi ya watu wanaamua kuficha fedha na hiyo inaathiri mtiririko wa fedha na wanaleta mfumuko wa bei, hawa sasa wanafanya hila kuzorotesha uchumi,” alisema Dk Bana na kuongeza kuwa kama fedha ni halali, kwa nini mtu afiche na kusema kuwa benki ndio mahali pekee salama kwa kutunza fedha na kama wapo watu wanatoa fedha benki na kuzificha majumbani wana hila za kuhujumu uchumi.

Alifafanua kuwa katika uhai wa taifa lolote kukiwa na mzunguko wa fedha wa kutosha katika jamii, husaidia kuimarisha thamani ya fedha na kwamba kama mzunguko huo utaathiriwa kwa makusudi unaweza sababisha hali mbaya ya uchumi.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa jambo la msingi la kufanya sio kuchapisha fedha mpya, bali ni kuhakikisha serikali inawabana wala rushwa na mafisadi ambao ndio wanachangia uchumi kuyumba.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania, Johnson Minja alisema wanaoficha fedha kwa makusudi ni wahujumu uchumi na wanapaswa kusakwa na kuchukuliwa hatua.

Minja alisema fedha sio mali ya mtu binafsi ni mali ya serikali na inapaswa kutumika kwa makusudi stahiki ambayo ni pamoja na kumwezesha mwananchi kufanya malipo mbalimbali na ndio maana fedha zote zina namba na saini ya waziri husika pamoja na gavana wa Benki Kuu.

“Watu waelewe kuwa fedha sio mali yao hata kama unazimiliki ni mali ya serikali na hupaswi kuzificha, ni lazima ziingie kwenye mzunguko wa fedha unapoficha ni kosa la kuhujumu uchumi na unapaswa kuchukuliwa hatua,” alisema Minja.

Alisema watu wanaoficha fedha nyumbani wengi wao ni wahalifu na wanafanya hivyo kwa sababu wanafahamu fedha hizo wamezipata isivyo halali na ni vyema vyombo vya uchunguzi nchini vikawamulika na kuwashughulikia kwa sababu wanahujumu uchumi kwa maslahi binafsi.

Hata hivyo, alisema pamoja ya kuwepo na tatizo hilo la baadhi ya watu kuficha fedha kwa makusudi, wapo pia wananchi walioficha fedha zao kwa sababu ya uelewa mdogo wa masuala ya fedha.

Alisema hivi sasa nchini kuna tatizo la kusuasua kwa mzunguko wa fedha unaosababishwa na kupanda kwa bei za kodi mbalimbali hivyo wananchi wana hofu ya kuagiza bidhaa nje kwa kuwa watashindwa kuuza kutokana na bei kuwa kubwa.

Alishauri serikali kuangalia jinsi ya kurudisha uchumi katika hali ya kawaida ili biashara zifanyike na watu waagize bidhaa nje.

Leave A Reply