The House of Favourite Newspapers

Wataalam Uganda watinga maonesho ya madini Geita, wapewa darasa teknolojia mpya uchimbaji madini

0
Mhandisi Uchimbaji Mwandamizi wa mipango kazi mirefu na wa chini ya ardhi kutoka GGML, Emanuel Njabugeni (kushoto) akiwaelezea wageni kutoka nchini Uganda namna GGML inavyotumia teknolojia mbalimbali katika uchimbaji wa wazi na wa chini kwa chini ya ardhi.

 

MAONESHO ya Teknolojia ya Madini yamezidi kuwa darasa kwa wadau mbalimbali baada ya wageni kutoka Wizara ya Madini ya Serikali ya Uganda kushiriki na kujifunza namna Kampuni ya GGML inavyotumia teknolojia za kisasa katika shughuli za uchimbaji wa chini kwa chini ya ardhi pamoja na wa wazi.

Wageni hao walioongozwa na Mkaguzi wa Migodi katika Kurugenzi ya Utafiti wa Jiolojia na Migodi anayesimamia shughuli za uchimbaji Mashariki mwa Uganda, Morris Muheirwe Tabaaro, walitembelea banda la GGML lililopo katika maonesho hayo ya sita yanayoendelea katika viwanja vya Bombambili-EPZ mjini Geita.

Akizungumzia dhumuni la kutembelea maonesho hayo, Tabaaro alisema mbali na kubadilishana uzoefu, pia wamekuja kujifunza namna kampuni hiyo inafanya utafiti wa madini, uchimbaji wa madini hiyo kwa njia za wazi na chini ya ardhi.

Aidha, akizungumzia darasa alililowapatia wageni hao kutoka Uganda, Mhandisi Uchimbaji Mwandamizi wa mipango kazi mirefu na wa chini ya ardhi kutoka GGML, Emanuel Njabugeni alisema hatua hiyo imedhihirisha kuwa Tanzania imezidi kuwa mfano wa kuigwa katika shughuli za uchimbaji kupitia miongozo mbalimbali iliyowekwa na hata kufikia dira ya Taifa.

Njabugeni mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 15 katika shughuli hizo za uchimbaji, alisema katika maonesho hayo, wameelekeza wageni, wachimbaji wadogo na washiriki kuhusu matumizi sahihi ya teknoliojia ambazo zinapunguza gharama za uchimbaji lakini pia kulinda mazingira.

“Tuna teknolojia ambazo zimepiga hatua ikiwamo software ya Studio UG for under ground Pamoja na teknolojia nyingine ambazo tumewaelekeza wenzetu wa Uganda namna zinavyoweza kuwapatia faida.

“Wenzetu wa Uganda wanayo haja kubwa kujifunza kutoka kwetu sisi watanzania hasa GGML ambayo ndio mgodi mkubwa Afrika Mashariki kwani unaongoza kiteknolojia na hata uhifadhi wa mazingira.

“Kwa hiyo nimewaelekeza ni kwa namna gani GGML inatumia teknolojia hizi katika kuchimba madini na kuhifadhi mazingira jambo ambalo limekuwa faida kwetu na hata jamii inayotuzunguka kwa ujumla,” alisema na kuongeza;

“Niliwaelezea kuwa kuna kampuni ambazo tunazitumia kwa ajili ya utafiti hapa Geita, mfano GGML tunatumia kampuni ya Capital Mining Services ambao wakishatupatia hizo data tunajua kwamba hapa tutachimbaji kwa faida au hasara. Kwa kuzingatia bei ya dhahabu, vifaa ambavyo tutavitumia na gharama za rasilimali watu na gharama mbalimbali kama kujaza mashimo na kuacha mwamba katika mazingira salama.”

Hatua hiyo inakuja wakati Serikali ikiendelea na jitihada za kutekeleza dira ya 2030 ambayo imeanzishwa na Waziri wa Madini, Athony Mavunde ambaye amelenga kuhakikisha madini yawe ni utajiri na maisha ya watanzania.

NA MWANDISHI WETU

Leave A Reply