The House of Favourite Newspapers

Watoto 2 Wanusurika Kufa Shangazi yao Akiwachoma Moto

0

KATIKA hali ya kusikitisha, watoto wawili wanaosoma darasa la kwanza Shule ya Msingi Mwanzumbi wilayani Igunga mkoani Tabora (majina yao yamehifadhiwa) wamenusurika kifo baada ya kuchomwa moto sehemu za mapaja na shangazi yao, Ashura Hamisi (31) kwa kosa la kurudi nyumbani usiku.

 

Wakizungumza kwa shida, watoto hao ambao wamelazwa Hospitali ya Wilaya ya Igunga wodi namba 8 jana, walisema walifanyiwa hayo na shangazi yao huyo ambaye amezaliwa tumbo moja na baba yao mzazi waliomtaja kwa jina moja la Maganga.

 

Walisema amekuwa akiwatuma kufanya biashara ya kuuza vitumbua mitaani ambapo Mei 9, mwaka huu, walikwenda kuuza vitumbua, lakini biashara haikuwa nzuri hali ambayo iliwalazimu kurudi usiku nyumbani.

 

Walisema baada ya kufika, shangazi yao alianza kuwafokea huku akiwatolea matusi ya nguoni ambapo wao waliamua kunyamaza na ndipo aliwakamata na kuwafungia ndani, kisha akachukua kisu na kukiweka kwenye jiko la moto.

 

Watoto hao walisema kisu hicho kiliposhika moto hadi kuwa chekundu  akakitoa kwenye moto na kuanza kumchoma mmoja-mmoja kwenye mapaja na kila kilipokuwa kikipoa kisu hicho yeye alikuwa akikirudisha kwenye moto.

 

“Mimi na mdogo wangu, tumenusurika kufa; shangazi alitutuma kwenda kumuuzia vitumbua mitaani kwa kubadilishana na mahindi lakini biashara haikuwa nzuri ndiyo maana tulirudi usiku, na yeye aliamua kutuchoma moto ili tufe ila Mungu mkubwa tunashukuru polisi kumkamata,” walisema.

 

Baadhi ya majirani, Jackson Samweli, Monica Athumani, na Hussein Joseph, walisema adhabu aliyoitoa kwa watoto hao ni ya kinyama kwa kuwa watoto hao walichomwambia ilitakiwa awasikilize ambapo wananchi hao wamelishukuru jeshi la polisi kwa kufanikiwa kumkamata mama huyo.

 

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Igunga, Merchades Magongo, alikiri kuwapokea watoto wote ambao ni kike ambapo mkubwa ana miaka kumi na mdogo ana miaka minane.

 

Alisema watoto hao waliwapokea Mei 10, 2020, wakiwa na majeraha makubwa ya moto na wamelazwa wodi namba 8 na hali zao zinaendelea vizuri, baada ya kupewa huduma ya matibabu huku mtoto mkubwa akiwa na majeraha makubwa.

 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Barnabas Mwakalukwa, alipoulizwa juu ya tukio hilo alithibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa.

 

“Polisi tulipokea taarifa kutoka kwa wananchi kuwa kuna mama mmoja anawachoma moto watoto wa kaka yake na ndipo polisi walifika kwa haraka katika eneo  na kufanikiwa kumkamata,” alisema.

 

Alisema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani wakati wowote kuanzia sasa na ametoa wito kwa jamii kushirikiana na dawati la jinsia la polisi kutoa elimu kwa ajili ya kukomesha vitendo vya kikatili dhidi ya watoto.

 

Alisema endapo jamii na taasisi za dini pamoja na wanasiasa wakishirikiana kutoa elimu katika maeneo yao ikiwa pamoja na kukaa na watoto wao kuwaelimisha juu ya kujiepusha na vitendo vibaya vya utukutu,  hali hiyo inaweza kutoweka.

Leave A Reply