The House of Favourite Newspapers

Wazambia Wavuruga Usajili wa Niyonzima

Wilbert Molandi | CHAMPIONI | Dar es Salaam

IMEFAHAMIKA kuwa, mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika itakayowakutanisha Yanga na Zanaco ya Zambia imevuruga usajili wa kiungo mchezeshaji wa Wanajangwani Mnyarwanda, Haruna Niyonzima. Timu hizo, zinatarajiwa kujitupa leo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam mchezo unaotarajiwa kujaa upinzani mkubwa.

Kiungo huyo, tayari yupo nchini na moja kwa moja alijiunga kambi ya pamoja kujiandaa na mchezo huo. Akizungumza na Championi Jumamosi, Niyonzima alisema mengi yamezushwa juu yake, lakini ukweli ni kwamba alirejea nyumbani kwao kwa ajili ya kuifanyia marekebisho hati ya kusafiria ‘passport’.

Niyonzima alisema, alirejea kuchukua hati hiyo nyumbani kwao Rwanda baada ya kupata ofa ya kwenda kucheza soka la kulipwa Cyprus. Aliongeza kuwa, amepanga kuelekea Cyprus mara baada ya mechi zote mbili ya hapa nyumbani na ugenini zitakapomalizika dhidi ya Zanaco, hivyo ameiomba klabu hiyo inayomhitaji kumsogezea mbele tarehe aliyopangiwa kwa ajili ya majaribio.

“Nilitakiwa hivi, sasa niwepo nchini Cyprus kwenye moja ya klabu, lakini mechi hii ya Zanaco imenivurugia, hivyo nimepanga kuzungumza na klabu hiyo leo (jana) kwa ajili ya kusogeza mbele tarehe niliyopangiwa kwa ajili ya majaribio.

“Ninatakiwa kuanza kufanya majaribio Machi 14, mwaka huu ambayo ni wiki ijayo tukijiandaa na safari ya Zambia katika mchezo wa marudiano, hivyo utaona jinsi gani ratiba itakavyokuwa imenibana.

“Ni vyema ikafahamika hivyo, lakini kiukweli mimi sikuwa na tatizo lolote kutoka kwa viongozi au shabiki kwa sababu mengi yalizungumzwa nilivyorudi nyumbani Rwanda kushughulikia matatizo yangu ya paspoti,” alisema Niyonzima.

Comments are closed.