The House of Favourite Newspapers

Waziri Malawi, washiriki kongamano la madini washuhudia ‘live’ uchimbaji GGML Geita

0
Waziri wa Madini kutoka Malawi, Monica Chang’anamuno, akipata maelezo mubashara kwa kutumia kifaa maalumu cha VR kuhusu shughuli za uchimbaji madini za kampuni Geita Gold Mining Limited (GGML) na mifumo ya kiteknolojia inayotumika ndani ya mgodi huo mkoani Geita. Kiongozi huyo alitembelea banda la GGML alipohudhuria Kongamano la Madini na Uwekezaji Tanzania lililofanyika jijini Dar es Salaam wiki iliyopita.

 

NA MWANDISHI WETU

KATIKA kuelimisha umma kuhusu teknolojia mpya na za kisasa zinazotumika kwenye sekta ya uchimbaji madini, Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imetoa fursa kwa washiriki wa Kongamano la Kimataifa la Madini na Uwekezaji Tanzania -2023 kutazama ‘live’ shughuli za uchimbaji zinazofanywa na kampuni hiyo mkoani Geita.

Washiriki hao wakiwamo viongozi mbalimbali wa serikali na waziri wa madini kutokea nchini Malawi, walipata fursa hiyo ya kujifunza katika kongamano hilo lililofanyika jijini Dar es Salaam kwa siku mbili wiki iliyopita.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini ya Malawi, Dk. Joseph Mkandawire akipata maelezo mubashara kwa kutumia kifaa maalumu cha VR kuhusu shughuli za uchimbaji madini za Kampuni hiyo ya GGML na mifumo ya kiteknolojia inayotumika ndani ya mgodi huo mkoani Geita. Kiongozi huyo alitembelea banda la GGML alipohudhuria Kongamano la Madini na Uwekezaji Tanzania lililofanyika jijini Dar es Salaam wiki iliyopita.

 

GGML ilitumia kifaa maalumu cha kutazama uhalisi wa matukio hayo kwa njia ya mtandao (Virtual Reality Headset) na kuwawezesha washiriki hao kujionea shughuli mbalimbali zinazoendeshwa na kampuni hiyo mkoani Geita kwa kutumia mifumo ya kisasa inayozingatia afya na usalama wa wafanyakazi mahala pa kazi.

Wakizungumzia teknolojia hiyo ambayo ilikuwa kivutio katika banda la GGML katika maonesho yaliyokuwa yanaendelea sambamba na kongamano hilo jijini Dar es Salaam Waziri wa Madini wa Malawi, Monica Chang’anamuno aliipongeza GGML kwa kuwa mfano wa kuigwa kutokana na matumizi hayo ya teknolojia hali inayorahisisha shughuli za uchimbaji madini nchini.

Mwanajiolojia Mwandamizi wa idara ya utafiti kutoka GGML, George Mwazembe akimuonesha Waziri wa Madini kutoka Malawi, Monica Chang’anamuno sampuli madini ya dhahabu yaliyoongezewa thamani. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini ya Malawi Dk. Joseph Mkandawire akisikiliza sambamba na Meneja Mwandamizi anayeshughuliki mahusiano ya jamii, Gilbert Mworia kutoka GGML. Viongozi hao wa Malawi walitembelea banda la kwenye Kongamano la Madini na Uwekezaji Tanzania, lililofanyika jijini Dar es Salaam wiki iliyopita.

 

Pia alitoa wito kwa kampuni hiyo kuendelea kushirikiana na serikali katika kukuza sekta hiyo ya madini ambayo ndio inayoongoza kwa kuingiza fedha za kigeni nchini.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Geita, Martin Shigela ambaye alikuwa mmoja wa washiriki waliotumia kifaa hicho kutazama uhalisia wa shughuli zinazoendelea mkoani Geita, alitoa wito kwa wawekezaji kuchangamkia fursa zilizopo katika mkoa huo hasa ikizingatiwa Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Maonesho hayo yaliyofunguliwa na Naibu Waziri Mkuu, Dk. Doto Biteko kwa niaba ya Rais Samia Suluhu Hassan tarehe 25 Oktoba 2023, yalifungwa tarehe 26 Oktoba 2023 na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa niaba ya Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi.

Leave A Reply