Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Afanya Ziara ya Kikazi Nchini Tunisia
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa ameondoka nchini kwenda Tunisia kwa ajili ya kumwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan katika mkutano wa nane wa wakuu wa nchi na serikali wa TICAD.
Taarifa kutoka ofisi ya waziri mkuu iliyotolewa jana ilsema kuwa mkutano huo utakaofanyika Agosti 27 mpaka tarehe 28 utatoa fursa ya kupanga mikakati ya ushirikiano na ajanda za maendeleo kati ya Japan na nchi za Afrika.
Kwa mujjibu wa taarifa hiyo Tanzania imekuwa ikishiriki mikutano hiyo tangu kuanzishwa kwake mnamo mwaka 1993, ambapo kupitia mikutano hiyo imekuwa ikifaidika kwa namna mbalimbali kama kujenga uhusiano mzuri na nchi za nje ambapo imepata misaada mbalimbali.
Kufuatia uhusiano mzuri kati ya Tanzania na Japan hasa kupitia shirika la kimataifa la maendeleo la Japan (JICA) Tanzania imekuwa ikinufaika na utekelezaji wa miradi mbalimbali katika sekta ya miundombinu ya Barabara, nishati, maji, elimu, afya na kilimo.
Afrika inashiriki katika mkutano huo kwa mara ya pili baada ya ule uliofanyika mwaka 2016 huko jijini Nairobi nchini Kenya.