The House of Favourite Newspapers

We baba fanueliii!!!-16

0

ILIPOISHIA

Mama Zubeda hakugundua kitu, simu haikutoa sauti, alipomaliza, akaificha na kumwambia amkalie kwa juu, tena huku akifumba macho kimahaba, mwanamke huyo pasipo kujua chochote, akafanya kila alichoambiwa, kilichofuata ni kupigwa picha tu huku akiwa ameyafumba macho yake kimahaba.

“Kwisha habari yake,” alisema mzee Paulo, akakenua, akaona kazi yake imekwisha.

TAMBAA NAYO

Baba Fanueli akaondoka nyumbani, hakuwa akienda baa kama alivyomuaga mkewe bali alitaka kuelekea nyumbani kwa kimada wake, Rose ambaye hakuwa akiishi mbali kutoka alipokuwa akiishi.

“Karibu mgeni,” alimkaribisha Rose.

“Asante. Mmmh! Umenona sana, yaani kupotea kidogo tu,” alisema baba Fanueli huku meno yote yakiwa nje, kwa jinsi alivyomwangalia Rose, alionekana kuwa mpya kwake.

“Haha! Hebu acha utani bwana. Nimekumisije!”

“Kweli?”

“Ndiyo!”

Baba Fanueli akaingia ndani, kitu cha kwanza, akapokelewa kwa mabusu mfululizo, akavuliwa shati lake na kubaki kifua wazi, kitambi hicho. Akakalishwa kitandani, bado mabusu yaliendelea kumiminika mashavuni mwake.

“Nikuandalie nini?” aliuliza Rose huku uso wake ukiwa umetawaliwa na tabasamu pana.

“Wewe unataka kuniandalia nini zaidi ya mapenzi? Hakuna kingine zaidi ya hicho, leo, nataka unipe mpaka nipagawe, tena unidatishe zaidi ya siku ile, utaweza?” aliuliza baba Fanueli, kila alipomwangalia Rose, kifua chake, kiuno na vitu vingine ambavyo vilifichwa na nguo laini aliyokuwa ameivaa, alibaki hoi.

“Hahah! Umeusahau ujuzi wangu, utamsahau mkeo…”

“Kweli?”

“Sasa subiri.”

Rose hakutaka kuandikia mate, alihakikisha anakuwa na wino wa kutosha, akamvuta vizuri baba Fanueli na kumlaza kitandani, akamtolea macho mithili ya jibwa koko lililomuona chatu.

Hata kabla baba Fanueli hajajiuliza ni nini kingefuata, akashtukia Rose akija juu yake na kuanza kusaula nguo zake na kubaki kama alivyozaliwa.

“Una swali?” aliuliza Rose huku akimwangalia baba Fanueli kwa macho ya mahaba.

“Mimi sina.”

“Sawa!” alisema Rose, kilichofuata ni kuanza kumpandisha chaji kwa kupeleka mikono yake huku na kule.

Wakati kila mmoja akiwa kwenye dimbwi la mahaba, mara simu ya baba Fanueli ikaanza kuita, iliwakera. Baba Fanueli aliona bora aipotezee lakini alipoona ikilia sana na kuwasumbua , akaichukua, kuangalia kioo, alikuwa mzee Paulo. Akaipokea.

“Vipi mzee mwenzangu?” aliuliza.

“Poa. Upo wapi nikupe mzigo wako?”

“Kwani tayari?”

“Ndiyo! Halafu nataka nisafiri, nimepigiwa simu mama anaumwa huko Rufiji,” alisikika mzee Paulo.

“Mmmh! Sasa hivi?”

“Ndiyo!”

“Aiseee! Haiwezi ikawa baadaye kidogo?”

“Kwani wewe upo wapi?”

“Nimetekwa hapa, yaani nipo katikati ya himaya ya mtu,” alijibu baba Fanueli.

“Achana naye kwanza, njoo tumalizane huku, halafu utaendelea naye, si unajua hii kazi ni lazima nikukabidhi,” alisikika mzee Paulo.

“Sawa. Ngoja nijitahidi,” alisema baba Fanueli.

Hakutaka kuuweka mahali hapo, japokuwa alikuwa kwenye tukio muhimu sana lakini kila alipofikiria aliona kwamba picha za mama Zubeda zilikuwa muhimu zaidi.

Akainuka kitandani pale, akavaa haraka mpaka Rose akabaki akimshangaa, mwenye hasira huku muda wote akiwa amekunja uso.

“Unakwenda wapi?”

“Si umesikia nimepigiwa simu,” alijibu baba Fanueli.

“Sawa. Kwa hiyo ndo’ unaniacha katika hali hii kweli?”

“Subiri, nitakuja hata baadaye, ngoja nikamuone huyu mtu kwanza,” alisema baba Fanueli, hakutaka kukaa sana, huyooo akaenda zake huku akiwa na kiherehere cha kupokea picha za adui yake, mama Zubeda.

 Njiani alionekana kuwa na presha kubwa, alijiona kuchelewa alipokuwa akienda, wakati mwingine alikuwa akikimbia, ilimradi tu awahi alipokuwa akienda.

“Upo wapi?” aliuliza mara baada ya kumpigia simu mzee Paulo.

“Nipo huku Machame Bar, wewe?”

“Nakuja, nipo njiani.”

Hakuchukua dakika nyingi, akafika katika baa hiyo ambapo akaangalia huku na kule, macho yake yakatua kwa mzee Paulo ambaye alikuwa kwenye meza na baamedi mmoja huku akimpigia ndogondogo, akamfuata.

“Karibu kaka…” alimkaribisha, akamruhusu baamedi yule aondoke huku akimgawia shilingi elfu kumi mpya kabisa.

“Tuonane baadaye,” alimwambia baamedi yule.

“Aya! Nimefika, nionyeshee,” alisema baba Fanueli huku akimwangalia mzee huyo usoni, alionekana kuwa na hamu ya kutaka kuziona picha hizo.

Mzee Paulo akachukua simu yake na kuanza kumuonyesha picha zile, aliziangalia, akakenua wee, uso wake ukajawa na tabasamu pana.

“Hapa safi, kama kazi imefanyika, hukuniangusha mzee mwenzangu,” alisema baba Fanueli.

“Usijali! Kwa hiyo inakuwaje?”

“Ndiyo nafikiria nini cha kufanya, kwanza ngoja, nitamfuata mimi mwenyewe kuzungumza naye, nikimwambia kuhusu hizi picha, atakoma na roho yake,” alisema mzee Paulo, akarushiwa zile picha kwa ‘bluetooth’ kisha kuondoka huku akiwa na hamu ya kuonana na mama Zubeda ili akinukishe.

Je, nini kitaendelea? Tukutane Alhamisi ijayo.

Leave A Reply