The House of Favourite Newspapers

Wewe unatoa sababu kibao za kukwepa unyumba…

0

Je, unazijua faida za kiafya za kufanya mapenzi?

NI Jumanne tena ambapo tunakutana kwa ajili ya mada katika safu hii. Ni safu yenye kutoa elimu ya maisha na mapenzi kwa ujumla.

Mada yangu ya leo imekwenda katika levo nyingine kabisa. Leo natoa elimu kuhusu faida zinazopatikana kwa binadamu kufanya tendo la ndoa.

KWANZA TUKUBALIANE HILI

Awali kabla ya kuendelea mbele, napenda kusisitiza kwamba, tendo la ndoa liliwekwa na Mwenyezi Mungu katika uhalali wake akiwakubalia wazazi wa dunia hii, Adamu na mkewe, Hawa au Eva.

Binadamu kwenye jinsia yake, akifikisha umri wa kuolewa au kuoa na kukutana kimwili na mwenzake wake, anakuwa anafanya tendo la ndoa, lakini pasipo uhalali inakuwa ni ngono na si tendo la ndoa tena.

Lakini kwa wale wenye uhalali ndiyo napenda kuwasemea zaidi katika mada hii. Wapo wanandoa wanaonyimana haki hiyo. Mimi najua. Lakini kama wangekuwa na uelewa kwamba, kuna faida zinazotokana na wanandoa kukutana kimwili au kufanya tendo la ndoa, kamwe wasingenyimana au kutoleana sababu dhaifu ili wasishiriki tendo.

Faida ambazo mtu anazipata kwa kushiriki tendo la ndoa ni kama ifuatavyo:

KUWEKA SAWA MFUMO WA KINGA YA MWILI

Mtu yeyote akiwa mahiri kwenye tendo la ndoa, anakuwa na kiwango cha juu cha kinga ya mwili wake dhidi ya virusi.

Wataalamu wanasema mtu akishiriki tendo hilo mara tatu au nne kwa wiki anakuwa na kiwango kikubwa cha kinga ya mwili ukimlinganisha na anayefanya chini ya hapo.

HAMU YA KUFANYA TENDO LA NDOA ZAIDI

Lakini faida ya pili kwa kufanya tendo la ndoa kwa kiwango hicho ni kuzidi kumfanya mhusika kuwa bora zaidi kwa tendo hilo kwa maana ya hamu ya kumudu kukutana mara kwa mara.

Kwa mwanamke tendo la ndoa kwa mara nne kwa wiki humsaidia katika mzunguko wa damu mwilini na pia humwongezea hamu zaidi ya kushiriki.

KWA WENYE TATIZO SUGU LA KUTOPATA USINGIZI

Wengi wanasumbuliwa na tatizo la kuusaka usingizi, lakini ni ukweli kwamba tendo la ndoa ni tiba kamili ya tatizo hilo. Kama unatafuta usingizi na upo na mwenzake wako, kutaneni kwa dakika hata tano na baada ya kufika kwenye kilele, usingizi wake unakuja bila kuutafuta kwa sababu tendo la kumaliza huita  homoni ya Prolacti ambayo hushughulika na usingizi.

HUPUNGUZA UWEZEKANO WA KUPATA SHINIKIZO LA DAMU

Uchunguzi wa kitaaluma unasema kuwa, kuna urafiki mkubwa kati ya tendo la ndoa na moyo kwani husaidia kupunguza shinikizo la damu.

HUPUNGUZA MAWAZO YA WIVU

Kama umebaini kuwa mwenza wako amekusaliti na ukapata ushahidi hivyo kuwa katika msongo unaotokana na wivu, ni tendo la ndoa pekee linaloweza kukuondoa katika msongo huo hasa baada ya kufika mwisho.

Kilele kwa vile kukumbatiana na kugusana kunaweza kusababisha kutolewa kwa homoni inayogusa hisia ya akili ya kujisikia vizuri.

NI MAZOEZI TOSHA

Lakini pia imebainika kwamba, kufanya tendo la ndoa mara kwa mara kuna faida kama zile zinazopatikana kutokana na mtu kufanya mazoezi kama ya kukimbia. Tendo la ndoa la mara moja na likadumu kwa dakika tano ni sawa na kukimbia kwa dakika 15 kuuzunguka uwanja wa mpira. Tendo la ndoa limefanikiwa kuupa moyo kasi ya kupiga vizuri.

HUONDOA HATARI YA MTU KUPATA MARADHI YA MOYO

Tendo la ndoa la mara nne kwa wiki husaidia kupunguza hatari ya mhusika kushambuliwa na maradhi ya moyo kama mshtuko.

Wanaofanya tendo la ndoa mara hizo kwa wiki, licha ya kuwa na uwezekano wa kufa kwa mshtuko wa moyo lakini si kama wale ambao hawafanyi mara hizo.

KWA WALE WENYE KUHISI MAUMIVU YA MWILI

Wapo wanaosikia maumivu ya miili na hivyo kutafuta dawa za kutuliza (pain killer), lakini kwa sababu si vizuri mwili kutumia dawa mara kwa mara, wajaribu siku moja wakati wa maumivu kushiriki tendo la ndoa kwani humaliza maumivu hayo haraka mara baada ya kumalizika kwa tendo.

MWANAMKE MWENYE MAUMIVU YA TUMBO LA HEDHI

Utafiti unaonesha kuwa, kwa mwanamke anayepata maumivu ya tumbo la hedhi, akisisimka mwili na kuwa tayari kwa tendo la ndoa, husaidia kuondoa maumivu hayo hata kama hatashiriki tendo. Tuonane wiki ijayo.

Leave A Reply