The House of Favourite Newspapers

Yanga Yamuandaa Tambwe Spesho Kwa Simba

YANGA imeweka wazi kwamba haitamtumia, Amissi Tambwe mpaka watakapojiridhisha kuwa hana pancha kabisa ingawa Spoti Xtra linajua kuwa wanamuweka fiti kwa mechi dhidi ya Simba. Mchezo huo wa watani wa jadi utakuwa wa nne kuanzia sasa baada ya mechi dhidi ya Ndanda, Mtibwa,Kagera na Stand United. Mchezaji huyo
ameanza mazoezi mepesi ambapo habari za ndani zinasema kwamba benchi la ufundi limeshauri asilazimishwe kucheza ili aimarike zaidi kwa mechi ngumu zijazo ikiwemo dhidi ya Simba.

 

Tambwe aliyefunga mabao 12 msimu uliopita tangu kuanza kwa msimu huu amekuwa na majeraha ya mara kwa mara ya goti ambayo yalimfanya kukosa michezo 11 ya mzunguko wa kwanza kabla ya kurejea kwenye mechi na Mbao FC ya Mwanza. Mwenyekiti wa kamati ya mashindano ya Yanga, Hussein Nyika ameliambia Spoti Xtra kuwa; “Kwa sasa hali za wachezaji wetu zinaendelea vyema na hivi karibuni Ngoma (Donald) amerejea kwenye timu na kuungana na wenzake kwa ajili ya kuanza mazoezi baada ya kuwa nje kwa kipindi kirefu.”

 

 

“Lakini kwa sasa tumeamua kumpa mapumziko ya muda mrefu mshambuliaji wetu, Amissi Tambwe kwa ajili ya kupumzika ili ajitibu vyema majeraha yake na atakapokuja kurejea basi awe vizuri na aweze kuipambania timu. “Kwa sasa hatoonekana uwanjani mpaka pale tutakapojiridhisha kwamba amekuwa vizuri kabisa kwa ajili ya kucheza ndipo atarejea tena kwenye timu kwa ajili ya kuungana na wenzake kuendelea kupambana kwa ajili ya kutetea ubingwa,” alisema Nyika ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya usajili ya timu hiyo. Tangu atue nchini Tanzania akitokea katika klabu ya Vital’O ya kwao Burundi, Tambwe tayari ameshafunga mabao 45 kwenye ligi kuu akiwa na klabu za Simba na Yanga. Mabao 25 ameyafunga akiwa Yanga na mabao 20 amefunga akiwa Simba

Comments are closed.