The House of Favourite Newspapers

Nanenane Dodoma Yaipaisha TZ Kimataifa – Video

0
Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Seleman Jaffo akipokewa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt. Anjelina Lutambi mara baada ya kuwasili kwenye viwanja vya maonesho ya Nanenane kanda ya kati Dodoma leo.kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi.

Mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano ya kuanzisha Maonesho ya Nanenane Kanda ya Kati Dodoma yameufanya Mkoa wa Singida kubuni na kuanzisha kilimo cha pamoja cha Korosho, zaidi ya ekari 25000 za pamoja.

 

Hatua hiyo imelifanya eneo hilo kuwa miongoni mwa maeneo makubwa ya kilimo hicho duniani ambalo litasaidia kuipaisha Tanzania katika uchumi wa kati wa juu na kuwa eneo maarufu la utalii wa kilimo duniani.

 

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti Mwenza wa Maonesho ya Nanenane Kanda ya Kati Mhe, Dkt. Rehema Nchimbi ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Singida kwenye ufunguzi rasmi wa maonesho hayo kwa mwaka huu.

 

Maonesho hayo ya kanda ya kati katika viwanja vya maonesho vya Nzuguni jijini Dodoma wakati akitoa salamu za Mkoa huo kabla ya kumkaribisha Mwenyekiti wa Kanda ya Kati Mhe, Dkt. Binilith Mahenge ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ili amkaribishe Mgeni Rasmi wa Maonesho hayo Mhe. Selemani Said Jaffo, Waziri wa TAMISEMI.

 

Dkt. Nchimbi amesema elimu iliyotolewa na taasisi mbalimbali za kilimo kwenye maonesho hayo ziliufanya mkoa uweze kuanzisha mashamba hayo makubwa kwenye Wilaya ya Manyoni, Ikungi na Itigi baada ya kupata msaada wa kitaalamu kutoka Bodi ya Korosho nchini na Watafiti kutoka chuo cha Kilimo cha Naliandele ambao wamefungua ofisi baada ya kuona kuwa kuna uhitaji wa kipekee wa kuwa hapo kutokana na tija kubwa ya zao hilo katika Mkoa wa Singida.

 

“ Kutokana na Mkoa wa Singida kuwa na mashamba makubwa ya Korosho natoa wito kwa wawekezaji wa viwanda vya kubangua Korosho kuja Singida ili kuwekeza kwani kutakuwa na malighafi ya kutosha na ya uhakika katika kipindi kifupi kijacho” alisisitiza Dkt. Nchimbi.

 

Ameongeza kuwa utafiti uliofanyika umeonesha Korosho za Singida zinauwezo wa kuzaa mara mbili kwenye msimu mmoja kutokana na hali ya hewa katika eneo hili na kwamba mkulima mmoja tayari amepata kilo 100 kutoka kwenye mkorosho mmoja kwa mwaka mmoja tu hali ambayo inaashiria zao hilo lina tija kubwa kwa wakulima.

 

Amesema kwa sasa Mkoa wa Singida unahamasisha “Nanenane Kaya” kwa maana ya kuwa kila kaya lazima kuzingatia maarifa yanatolewa na wataalam kwenye maonesho ya nanenane kanda ya katika maeneo ya kilimo, mifugo na uvuvi ili kuongeza kipato.

Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Seleman Jaffo (mwenye suti nyeusi na tai) akiwa na viongozi wakuu wa Mkoa wa Dodoma na Singida akikata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa maonesho ya Nanenane kanda ya Kati Dodoma kwenye viwanja vya Nzuguni leo.

Ameongeza kuwa kwa sasa mkoa unajipanga kuongeza zao la Parachichi ambapo amesema tafiti zinaonyesha kuwa ardhi ya Mkoa wa Singida inafaa kwa kilimo cha zao hilo na kwamba kinachotakiwa ni kupata maji ya kutosha kwa ajili ya umwagiliaji wa zao hilo.

 

Ampongeza Rais John Pombe Magufuli kwa kuiingiza Tanzania kwenye uchumi wa Kati na kuwaomba watanzania kumchagua tena katika kipindi kijacho ili maono yake ya kuhakikisha uchumi wa nchi unakua kwa kasi itimie.

 

“Kwa mkoa wa Singida tumejipanga kuhakikisha tunaunga mkono jitihada hizo kwa kufanya kazi kwa bidii na kutangaza fursa mbalimbali za uwekezaji katika mkoa huo,” alisema.

 

Awali akizungumza Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Anjelina Lutambi amezitaja fursa zinazopatikana kwenye Mkoa huo kuwa ni pamoja na viwanda vya kuchakata mazao ya mifugo,viwanda vya kukamua mafuta ya alizeti na karanga,viwanda vya kusindika asali,ranchi za mifugo na kilimo cha vitunguu.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Dkt. Rehema Nchimbi (mwenye kilemba) akishiriki kucheza Ngoma za Utamaduni za kikundi cha Chuo Kikuu cha Dodoma wakati wa ufunguzi rasmi wa maonesho ya Nanenane kanda ya kati Dodoma wakati Mgeni rasmi Mheshimiwa Seleman Jaffo Waziri wa TAMISEMI (mwenye suti) akikagua vikundi hivyo.

Vingine ni viwanda vya kuchakata bidhaa za maziwa,viwanda vya kutengeneza chakula cha samaki na mifugo,viwanda vya kutengeneza mvinyo,viwanda kutengeneza jasi (gypsum),viwanda vya kuchakata korosho na uchimbaji wa madini na mafuta.

 

Aidha Mwenyekiti wa maonesho hayo Kanda ya Kati Dkt. Mahenge alimwomba Mgeni Rasmi Mhe. Jafo kuiomba Serikali katika mwaka ujao kufanyia maonesho ya Nanenane kitaifa katika viwanja vya Nzuguni kwa kuwa ndiyo makao makuu ya nchi na kwamba uwanja huo unakidhi vigezo vyote ambapo Mhe. Jaffo alikubali kuwasilisha ombili hilo Serikalini.

 

Akifungua maonesho hayo ya Kanda ya Kati Waziri Jaffo amewataka wananchi kutumia maarifa yanayotolewa na wataalam ambapo amesema bado hayajatumika kikamilifu na kuagiza maafisa ugani kote nchini kuhakikisha wanawasaidia wananchi kulima na kufuga kisasa.

1Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Seleman Jaffo (mwenye suti nyeusi na tai) akiwa na viongozi wakuu wa Mkoa wa Singida na Dodoma wakipata maelezo ya kilimo cha mtama kutoka kwa mtaalam wa Wizara ya Kilimo kwenye viwanja vya Nzuguni -Dodoma wakati wa ufunguzi wa Maonesho ya Nanenane Kanda ya Kati.

“Tuna fursa kubwa ya kujenga nchi yetu kwa kutegemea Kilimo, Mifugo na Uvuvi” amesisitiza Jaffo

Amepongeza kuwa na paredi la mifugo kwenye maonesho ya mwaka huu na kuelekeza kila Halmashauri nchini kuhakikisha inatenga maeneo ya kutosha ya malisho.

 

Aidha amempongeza Katibu ya Kamati ya maandalizi ya maonesho hayo kanda ya kati Bi Aziza Mumba ambaye ni Katibu Tawala Msaidizi anayesimamia Sekta ya Uchumi Mkoa wa Dodoma, pamoja na Kamati yake kwa maandalizi mazuri ya mwaka huu ambapo ameitaka kamati hiyo kufanya maandalizi mazuri zaidi katika miaka ijayo ili wananchi wanufaike zaidi na maarifa yanayotolewa.

Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Seleman Jaffo (mwenye suti nyeusi na tai) akipata maelezo ya uhimilishaji wa mifugo kutoka kwa mtaalam wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, nyuma ni Mwnyekiti wa Maonesho ya Nanenane kanda ya kati, Mhe. Dkt Binilithi Mahenge Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, kushoto ni Bi. Aziza Mumba Katibu wa Kamati ya Maandalizi. (Picha na John Mapepele)

Bi. Mumba amesema Kamati yake imepokea na itahakikisha kuwa inasimamia na kutekeleza maagizo hayo kikamilifu ikiwa ni pamoja na kuboresha mapungufu yote yaliyojitokeza mwaka huu.

 

Mwaka 2020 ni mwaka wa kumi na tatu (13) katika kufanyika kwa maonesho ya nanenane katika viwanja vya Nzuguni na ni mara ya Kumi (10) kuendelea kufanya mashindano maalum ya paredi la mifugo ili kushindanisha mifugo bora.

 

Leave A Reply