The House of Favourite Newspapers

Zijue Sababu Sugu Zinazochangia Kuachwa Mara kwa Mara

Duma

Na DAUDI MICHAEL ‘DUMA’| GAZETI LA AMANI| UHUSIANO, ELIMU, MIGOGORO, MAPENZI| MAKALA

HABARI yako! Mpenzi msomaji wiki jana kwenye Sindano za Mastaa tulikuwa na mwigizaji wa filamu za Kibongo, Pili Lwey ‘Mama Nyamayao’ ambaye alitupa sindano zake za mahaba ambazo zilituingia vilivyo. Wiki hii pia tunaye msanii wa filamu za Kibongo,

Daud Michael almaarufu Duma ambaye anakufungukia sababu sugu ambazo zinaweza kukufanya uachwe au ukaachana na kila mpenzi unayempata, ungana naye. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kunitunuku nafasi ya kuweza kujadiliana nanyi mashabiki wangu na wasiyo mashabiki kuhusu changamoto mbalimbali zilizopo kwenye uhusiano wa kimapenzi.

Hivi ulishawahi kujiuliza ni kwa nini kila siku wewe umekuwa ni mtu wa kuachwa na kila mpenzi unayempata?

UBABE WAKO

Ubabe ni chanzo kikubwa cha mifarakano katika uhusiano wa kimapenzi. Utakuta mwanaume ni mbabe kupitiliza kwa mpenzi, mchumba au mkewe, mwanamke au mwanaume asifanye jambo dogo, ameshamtolea bonge la tusi, asifanye hivi kapewa teke! Hili ni tatizo. Kila siku utaishia kubadilisha wanaume au wanawake kwa sababu ya tabia zako za ubabe. Mapenzi hayahitaji ubabe bali lugha yenye mnato na mvuto kwa mwenza wako.

UZURI WAKO

Baadhi ya wapenzi ambao wanajifahamu kuwa wao wamebarikiwa, wamejaliwa kuwa na umbo au sura nzuri, basi kila kitu anachokifanya, anafanya kwa kujishebedua, akiamini kuwa mpenzi wake hana cha kumfanya kwa sababu ameumbika vizuri au kwa sababu yeye ni mtanashati. Tabia hiyo ya kujiona mzuri, humfanya kuleta uzuri ule hadi faragha, jambo ambalo halistahili. Wewe nani amekuambia uzuri wako ni muhimu kwenye sita kwa sita? Pale panahitaji kazi tu na si mbwembwe kama zako, ndiyo maana unaweza kumkuta msichana mrembo au kijana mtanashati lakini hadumu na mpenzi anayempata kwa sababu ya tabia yake ya umimi.

KUTOKUJIWEZA FARAGHA

Shindwa kazi yoyote, shindwa chochote katika dunia hii ila usishindwe kumpa huduma nzuri, yenye kumridhisha faragha mpenzi wako. Kama utakuwa unaweza kufanya mambo mengine vizuri lakini faragha unakuwa hujiwezi, hili ni tatizo kubwa sana, tatizo ambalo unatakiwa kulitafutia utatuzi mapema. Uvivu au kutokujituma unapokuwa faragha na mweza wako inaweza kuchangia kwa asilimia kubwa zaidi kuachwa na kila mpenzi unayekuwa naye. Mbaya zaidi uvivu wa faragha haubebwi na uzuri, elimu, umri, fedha, ustaa, wadhifa au umaarufu ulionao katika jamii.

URITHI WAKO

Mali za urithi nazo ni tatizo sana kwani utakuta mtu anatumia urithi wake kumnyanyasa mpenzi wake. Kwa mfano, mwanamke aliachiwa nyumba na wazazi wake na anakuwa na uhusiano na mpenzi wake, anaamua kuishi kwenye nyumba yake lakini utakuta anajisahau nakutaka kumpanda kichwani mpenzi wake. Anajikuta akisahau kuwa yeye ni mwanamke na mwenziye ni mwanaume pamoja na kwamba walikubaliana kuwa wataheshimiana na kupendana kwa dhati! Hilo jipu uchungu. Lazima jamaa atakukimbia kwani ataona kama unamnyanyasa kutokana na kipato, elimu, uwezo wako na kadhalika. Hivyo unapaswa kuwa makini sana na sababu hizo ambazo nimeziandika hapo na sababu hizi ni kwa wanawake na wanaume.

MAJIVUNO/KUJISIKIA

Hili pia ni tatizo kwenye uhusiano, haiwezekani wewe uwe ni mtu wa kujisikia au kujivuna kuwa wewe ni bora kuliko mweza wako, mtu unaishi naye, ‘unashea’ naye kila kitu lakini unamdharau, haipendezi na kwa tabia hiyo huwezi kudumu na mpenzi kwa muda mrefu kwani kila mtu atakuwa anakukimbia kwa sababu anajua hujui thamani ya kupenda. Kwa leo ninaishia hapa, usikose kupitia ukurasa huu wiki ijayo maana utakutana na mada nyingine nzuri ambayo itakupa mafunzo ya kutosha. Je, unapenda msanii gani atoe somo la Sindano Za Mastaa wiki ijayo? Tuma maoni na ushauri kupitia namba 0679979785.

 

SHINDA NYUMBA AWAMU YA PILI YATIKISA JIJI LA DAR ES SALAAM

Comments are closed.