The House of Favourite Newspapers

Lile La Lissu Karia Alichemsha, Lakini Lisigeuke Fimbo…

Rais wa shirikisho hilo, Wallace Karia.

WAKATI wa Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), rais wa shirikisho hilo, Wallace Karia alizua taharuki kutokana na kuzungumza mfano ulioingiza soka la Tanzania katika siasa.

 

Karia alimtaja mwanasiasa maarufu nchini, Tundu Lissu ambaye alikuwa kwenye matibabu nchini Ubelgiji. Wakati wa mkutano huo, ilionekana Karia akimzungumzia aliyekuwa Makamu wa Rais wa TFF, Michael Wambura.

Alikuwa akielezea kwamba Wambura amekuwa akizunguka huku na kule kuichafua TFF kama anavyofanya Lissu ambaye amekuwa akizunguka katika vyombo vya habari mbalimbali maarufu vya Ulaya.

 

Ukiangalia Karia alitaka kusherehesha au kukielezea vizuri alichokuwa anakisema. Lakini inawezekana alijikuta akitoa yake ya moyoni bila kutarajia.

 

Hakuna anayeweza kuungana naye kusema siasa iingie katike michezo jambo ambalo si sahihi na halitakubalika.

 

Kitu kizuri zaidi ni kwamba Karia mwenyewe ameliona hilo na amekubali kuomba radhi kwani baada ya mkutano tu, alitoka nje na kusema alikuwa akieleza jambo kama maoni lakini kama amewakwaza watu, basi wamuwie radhi.

Hili lilikuwa jambo zuri zaidi baada ya lile. Kama angekaa kimya na kukataa kuomba radhi, maana yake angeonyesha alijipanga kufanya alichotaka kufanya bila ya kujali.

 

Uamuzi wake wa kusema anaomba radhi kwa aliowakwaza, maana yake anakubaliana na mimi na wewe kuwa alikosea, hakutarajia na pia hakubaliani na siasa kuingizwa michezoni.

 

Bila shaka hili ndilo tunalotaka. Tuweke mpaka, watu wa siasa tuwaache pembeni na watu wa michezo tuendelee na mambo yetu wenyewe.

 

Wakati wa kuunganika na watu wa siasa upo, hasa pale wanapoalikwa kuwa wageni rasmi au nao wakiamua kujivua uanasiasa na kuungana nasi michezoni. Hilo linakuwa halina shida hata kidogo.

Hivyo, Karia ameliona, amekuwa muungwana na kuomba radhi. Nafikiri ni jambo jema kwa ambaye anakosea na kuweza kuona.

 

Naona itakuwa kazi kidogo mjadala huu kwisha kwa kuwa kila mmoja ana aina yake ya kujadili mambo. Mmoja haraka na kufikia uamuzi, mwingine taratibu na kuendelea kujadili tena na tena.

 

Huwezi kumzuia mtu kuendelea kujadili au la, kama ambavyo najadili hapa nanyi. Lakini vizuri kwa wanaojadili kutoifanya TFF haina ilichofanya, au mbaya sana sababu tu ya kauli hiyo.

 

Kauli hiyo kweli amekosea kiongozi wake, lakini haina maana kukosea huko tuonyeshe TFF haifai kabisa, haijawahi kufanya lolote na haina msaada wowote.

Kama litakuwa ni suala la TFF haijafanya lolote, basi kuna haja ya kuonyesha kupitia data nyingine ambazo ni sahihi na si suala la Lissu.

 

Tusichanganye mambo kwa kuwa inawezekana baadaye wanaolaumu ndiyo wakawa wanachanganya siasa na michezo kwa kutaka kufanya mwendelezo wa muda mrefu bila ya sababu.

Kama muhusika amekiri amekosea, wakati mwingine unapaswa kumuona muungwana. Anayesema kama kuna niliowakwaza, wanisamehe. Sasa kipi kingine zaidi alitakiwa kusema.

 

Suala la kuingiza vitu vingi, kuonyesha TFF haifai, TFF imefeli kwa sababu ya kauli yake, inaonyesha udhaifu kwa watoa hoja. Badala yake kama wanajua kuhusiana na hilo, wako huru na waweke hoja inayoonyesha kweli wamefeli na wadau tujadili tukiwa huru kwa nia njema.

 

Karia amekosea, ameomba radhi. Sasa hatuna haja ya kuendelea kukosea zaidi na kuisimika siasa katika michezo. Tunaweza kuwaachia wataalamu wa hayo mambo nasi tuendelee na yetu ambayo bado yana upungufu wa mengi tunayopaswa kuyafanyia kazi.

 

Kikubwa zaidi ni kuamini, Karia atakuwa amejifunza sana katika suala hilo lakini atakuwa amewafundisha wanamichezo wengi kwamba wawe makini na wao siku moja wasiteleze na kuzua taharuki.

 

Namna wanamichezo w a l i v y o o n y e s h a kutofurahishwa na hilo, wameonyesha wazi hawataki tasnia waliyomo ichanganywe na siasa ambalo ni jambo zuri na tunapaswa kulishikilia.

Comments are closed.