The House of Favourite Newspapers

Fei Toto amuwahi Sure Boy Azam FC

KIUNGO fundi wa Yanga, Feisal Salim ‘Fei Toto’ amemaliza adhabu yake ya kadi tatu za njano na anatarajiwa kurejea uwanjani kwenye mchezo ujao wa Ligi Kuu Bara watakapovaana na Azam FC yenye viungo nyota kama Salum Abubakary ‘Sure Boy’.

 

Fei Toto aliukosa mchezo uliopita wa ligi Yanga walipocheza na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri huko mkoani Morogoro ambao ulimalizika kwa kufungwa bao 1-0.

 

Kiungo huyo, anatarajiwa kurejea kwenye mchezo dhidi ya Azam utakaopigwa Aprili 29, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Meneja wa Yanga, Hafidh Saleh alisema kuwa kiungo huyo anatarajiwa kuwepo kwenye sehemu ya wachezaji watakaowavaa Azam.

Saleh alisema, kiungo huyo amemaliza adhabu ya kuukosa mchezo mmoja wa ligi kutokana na kadi tatu alizozipata kiungo huyo anayemudu kucheza namba 6, 8 na 10.

 

“Mchezaji ambaye anatarajiwa kuukosa kwenye mchezo ujao dhidi ya Azam ni Yondani (Kelvin) pekee ambaye yeye bado anatumikia adhabu ya kadi nyekundu ya moja kwa moja.

 

“Kadi hiyo inamfanya aikose michezo mitatu ya ligi ambayo aliipata kwenye mchezo wetu na Kagera Sugar, katika mchezo huo, pia Fei Toto alipewa kadi ya njano na kufikisha kadi tatu za njano.

 

“Hivyo, Fei Toto tayari amemaliza adhabu yake ya kuukosa mchezo mmoja tulipocheza na Mtibwa Sugar, hivyo kwenye mechi yetu dhidi ya Azam atakuwa sehemu ya kikosi chetu,” alisema Saleh.

Comments are closed.