The House of Favourite Newspapers

Adakwa akienda kutupa kichanga!

0

IMG-20151216-WA0001 Kichanga kilichotaka kutupwa  na mama yake.

Deogratius Mongela na Chande Abdallah
INASIKITISHA! Wakati watu wengi wakisaka watoto kwa udi na uvumba, mama anayejulikana kwa jina la Ruth, mkazi wa Mbezi jijini Dar amenusurika kichapo kutoka kwa wananchi baada ya kumdaka akiwa kwenye harakati za kutaka kumtupa mtoto baada ya kujifungua.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio, siku ya tukio, Desemba 14, mwaka huu, majira ya saa 2 asubuhi, walimuona Ruth ambaye alikuwa mjamzito akilalamika kuwa tumbo linamsokota ndipo majirani wakataka kumpeleka hospitali wakiamini huenda tarehe za kujifungua ziliwadia.

IMG-20151216-WA0004Mmoja wa majirani anasema kuwa wakati wakijiandaa kumpeleka hospitali, walishangaa kutosikia tena kelele za maumivu huku kilio cha mtoto mchanga kikisikika jambo lililoashiria kuwa alikuwa amejifungua pale nyumbani.

“Ghafla nilisikia kama mlio wa mtoto, niliposogea kutaka kujua nini kinaendelea, mlango ulifunguliwa na akatoka rafiki yake nikamuulizia kuhusu Ruth akaniambia amepumzika ndani na akaniambia amejifungulia ndani kwake kwa kushirikiana na rafiki yake,” alisema mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo.

Kama hiyo haitoshi shuhuda huyo alidai kuwa pamoja na kujifungua salama, Ruth alionesha azma ya kutaka kumtupa mtoto wake ambapo alimtaka rafiki yake huyo amsaidie kutekeleza unyama huo.

IMG-20151216-WA0002

Mtuhumiwa aliyetaka kutupa kichanga hicho.

“Aliniambia nimsaidie kumtupa mtoto wake lakini nikamwambia siwezi kushiriki unyama huo, katoto kenyewe kazuri kweli halafu huwezi amini anataka kukatupa! Nikamkimbia kwenda kumwambia mjumbe ili tuweke mtego na kweli alikamatwa usiku huohuo akielekea kumtupa mtoto vichakani,” alisema rafiki wa Ruth aliyeomba hifadhi ya jina lake.

Waandishi wetu walimtafuta mjumbe wa eneo hilo, Devotha Constatino aliyehusika katika kumnasa mama huyo akiwa mbioni kukitupa kichanga chake ambaye alisema kuwa alipata taarifa za Ruth kujifungua kwa siri na kutaka kumuua mwanaye kwa kumtupa pindi jua litakapozama.

“Tuliweka mtego na kweli tulimnasa akiwa na mtoto ndani ya beseni huku akiwa amemshindilia na matambara, alikuwa akijitetea kuwa mimba yake imeharibika lakini tulipomkagua mtoto alikuwa akipumua vizuri tu.

IMG-20151216-WA0009“Hapo ndiyo wananchi wenye hasira walitaka kumpiga, tukamuokoa na kumpeleka Kituo cha Polisi kwa Yusuph lakini cha kushangaza polisi walisema hawawezi kumshikilia Ruth kwa kuwa mtoto hakufariki.

Tulichokifanya ni kumpeleka yeye na mtoto wake mpaka Hospitali ya Tumbi Kibaha kwa Matibabu na kumuonya,” alisema mjumbe huyo.

Leave A Reply