Azimio Wamlaumu Rais Kenyatta Kumuangusha Raila Odinga Urais Kenya
WANASIASA wa muungano wa Azimio la Umoja One Kenya, sasa wameanza kumlaumu Rais Uhuru Kenyatta huku wakidai alisababisha mgombea wao wa urais Raila Odinga kuanguka kwenye uchaguzi uliofanyika Agosti 9.
Baadhi ya wanasiasa ambao wanamtupia jicho la lawama Kenyatta ni aliyekuwa Mbunge wa Starehe, Maina Kamanda, Katibu Mkuu wa Chama cha Kitaifa cha Wafanyakazi (Cotu) Francis Atwoli, wabunge Babu Owino (Embakasi Mashariki), Caleb Amisi (Saboti) na Seneta wa Narok Ledama Olekina kati ya wengine.
Wanasiasa hao wanamlaumu Rais Kenyatta kwa kupuuzia ushauri na miongozo aliyopewa, huku wengine wakimpa sifa Rais Mteule William Ruto kwa kuwa na ujuzi wa kipekee wa kisiasa, hali iliyomwezesha kuwapiku na kuibuka kidedea katika kinyang’anyiro cha Urais.
Mnamo Ijumaa, Bw Kamanda alidai kuwa hatua ya Rais Kenyatta kukataa ushauri wa viongozi waliomzidi umri ndani ya Azimio, ilisababisha kuanguka kwa Bw Odinga.
Vilevile, alisema uchaguzi huo ulikuwa huru pia wa haki jambo ambalo linapingwa na viongozi wengi wa Azimio, wakisema kuwa uchaguzi huo ulikumbwa na visa vya udanganyifu na wizi wa kura.
Imeandikwa na: Oswald Mwesiga kwa Msaada wa Mitandao.