DAR ES SALAAM: MWENYEKITI mpya wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Semistocles Kaijage, anayeshika nafasi iliyoachwa wazi na Jaji Mstaafu Damiani Lubuva aliyemaliza muda wake Desemba 19 mwaka huu amesema kuwa katika msingi wa uongozi wake anategemea kutenda haki kwa kuzingatia sheria na taratibu za kiapo alichoapishwa leo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.John Pombe Magufuli.
Ameyasema leo wakati alipoulizwa swali na mwandishi wa habari katika ofisi za NEC jijini Dar es Salaam wakati akitoa taarifa juu ya kufanyika kwa uchaguzi mdogo wa ubunge na madiwani utakaofanyika Januari 22,2017.
AlisemaTume ya Taifa ya Uchaguzi kwamujibu wa kifungu cha 37 (1)b cha sheria ya Taifa ya Uchaguzi, sura ya 343 ilitangaza kufanyika kwa uteuzi wa wagombea wa uchaguzi huo Desemba 22 mwaka huu ambapo jumla ya vyama vyenye wagombea kwa jimbo la Dimani, Zanzibar, ni 11 na wote wakiwa ni wanaume.
“Kwa upande wa udiwani, katika halimashauri 20 za Tanzania bara, vyama vyenye wagombea ni 13. Jumla ya wagombea wa nafasi ya udiwani ni 72 na kati ya wagombea hao wanawake ni watano na wanaume 67.
“Hadi sasa pingamizi zilizokatwa ni sita, ambapo tano zimekatwa kwenye kata ya Ihumwa Manispaa ya Dodoma na moja katika kata ya Isagehe Halmashauri ya Mji wa Kahama.
Aidha alifafanua kuwa kwa mujibu wa ratiba ya uchaguzi tayari kampeni zimekwaishaanza leo na zinategemea kufikia mwisho Januari 21,2017 na kamati za maadili zinaendelea kuundwa katika ngazi mbalimbali ambapo zitakuwa na jukumu la kusimamia utekelezaji wa maadili katika kipindi chote cha kampeni.
Na Denis Mtima/GPL
MWENYEKITI NEC, BAADA YA KUAPISHWA AAHIDI KUTENDA HAKI KWENYE UCHAGUZI
Comments are closed.