The House of Favourite Newspapers

Banda Ana Jambo Lake Simba Day

0

WINGA wa Simba, Mmalawi, Peter Banda, amesema kuwa atafurahi kuona mashabiki wa Simba wakiujaza Uwanja wa Mkapa katika mchezo wao watakaocheza dhidi ya TP Mazembe siku ya Simba kwani wao kama wachezaji wamewaandalia zawadi nzuri ambayo ni mchezo mzuri dhidi ya wapinzani hao.

Simba, leo Jumapili, wanatarajiwa kuadhimisha kilele cha siku ya Simba ‘Simba Day’. Watacheza mchezo wa kirafiki dhidi ya TP Mazembe kutoka DR Congo. Katika siku hiyo, mashabiki wa Simba hupata nafasi ya kutambulishwa wachezaji wote ambao wamesajiliwa na timu hiyo kwa ajili ya msimu ujao.

Akizungumza na Championi, Banda alisema kuwa wao kama wachezaji wamepanga kuwaonyesha mchezo mzuri pindi watakapocheza na TP Mazembe, hivyo anatamani kuona mashabiki wakija kwa wingi kuiunga mkono timu yao katika siku yao ya Simba.

“Ni siku nzuri kwa familia nzima ya Simba, kwa jinsi ambavyo naona, ingawa sijawahi kulishuhudia tamasha hili likifanyika lakini linaonekana kuwa ni tamasha kubwa kutokana na shauku ya kila Mwanasimba kutamani siku ya tukio ifike.

“Wachezaji wenzangu ambao tayari wamewahi kushiriki wananielezea siku hii kwa ukubwa jambo ambalo natamani liendelee kila mara ndio maana natamani kuona mashabiki wakija kwa wingi siku hiyo na sisi wachezaji hatutawaangusha kwani tutajitahidi kuwaonyesha mpira mzuri dhidi ya wapinzani wetu,” alisema Banda.

Marco Mzumbe, Dar es Salaam

Leave A Reply